Wednesday 8 March 2023

MWANANGU ! UKIFIKA UGENINI ZINGATIA MAMBO HAYA ILI UFANIKIWE 

 MWANANGU ! UKIFIKA UGENINI ZINGATIA MAMBO HAYA ILI UFANIKIWE 

Kila mtu kwa sehemu ni lazima kawahi kuwa mgeni au atakuwa mgeni tu siku moja,kuwa mgeni haiepukiki kila mtu ni lazima atapitia, yawezekana ni ajira mpya au kutoka nyumbani kwenda mkoani kutafuta maisha. Wengi tukifika ugenini huwa tunajikuta kwenye migogoro mingi na wenyeji kiasi cha kuchukia kabisa eneo hilo na hatimaye kushindwa kufanikisha lengo kuu lililotupeleka ugenini, Uhaba wa ufahamu wa mbinu za kuishi ugenini ni sababu kubwa za yote hayo ndio maana nikaona nikuandalie machache yatakayokusaidia kuishi ugenini kwa mafanikio makubwa.Ukifika ugenini zingatia haya :

1.Usifike ukawa mjuaji kuliko wenyeji uliowakuta kwani watashindwa kukuonyesha hata kisima cha maji kilipo.

2.Usifike na kuanza kukosoa wenyeji kwani wataona unawadharau.

3.Usifike ukaanza kudharau kabila la wenyeji tena hili ni kosa kubwa ukifika epuka maongezi yanayotaja makabila ya watu au kutolea mifano makabila ya watu.

4.Ukifika tafuta nyumba ya ibada na jumuiya jiunge huko kwa sababu watakaokusaidia kwa huduma ya kwanza ni hao wenyeji na sio kwenu ulipotoka , hata kama kwenu wana uwezo vipi wa kifedha lakini kuna shida zako nyingine wao watakwama lakini wenyeji wako watazimudu. 

5.Usianzishe mahusiano ya kimapenzi haraka haraka, kuwa mtulivu.Hata kama umefika na ukamuona mtoto wa mtu ukampenda sana jitahidi ujizuie tena hapo jizuie haswa kwa sababu hujui mengi kumuhusu huyo binti yawezekana asiwe na shari yoyote lakini kumbe tayari ni mchumba wa mtu hapo ugenini hivyo ukajikuta kwenye vita na wenyeji na huwezi kuishinda hiyo vita kwa sababu utapigana na wanaojua ghara za silaha zilipo. 

7.Usionyeshe ukubwa wako acha waone kwa vitendo.Usifike ugenini ukaanza kuonyesha ukubwa wako au ukaanza majisifu wewe fanya kilichokupeleka kwa weredi na bidii zote na kama una huo ukubwa basi utaonyeshwa na juhudi zako.

8.Acha wenyeji watawale mazungumzo hata kama unaongea kama chiriku jizuie 

9.Usiwaonyeshe kuwa wewe ni bora zaidi yao hata kama ni kweli jifanye tu mwanafunzi hata kama wewe ni mwalimu.

10.Usinunue ugomvi acha wachukiane wao wewe kaa pembeni Ukifika utaanza kuonyeshwa nani mbaya na nani mzuri tafadhali usikurupuke kuunga mkono upande mmoja wapo bali tulia tu na baadaye utajionea mwenyewe nani anafaa na nani hafai. 

11.Hata kama una pesa anza kwa kula vyakula vyao 😄 Namaanisha ndio usifike ukaanza kuona kama vile vyakula vyao havifai na hata kama wanatumia usichoweza kula basi usikatae kwa dharau bali tumia hekima kubwa kufikisha ujumbe kuwa chakula chao ni kizuri sana na tena unasikitika kukikosa lakini huna namna inabidi tu ukikose.

12.Una elimu kubwa ndio lakini ukifika ugenini usigombanie uongozi ,wenyeji watakuchukia haraka watajua umeenda kuharibu maslahi yao .Ukifika kubali kuongozwa na tii kila kiongozi wako bila kujali unamshinda nini, baadaye wakiona unafaa wao wenyewe watakupa uongozi.

13.Sio lazima uwe kiongozi eneo hilo yawezekana nafasi yako nzuri ni kuwa mshauri wa viongozi wa eneo hilo.


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha. 


#kitabu cha thamani ya changamoto kinapatikana nakala tete ( soft copy)

+255652 134707




#kitabu cha thamani ya changamoto kinapatikana 

+255652 134707