Friday 22 March 2024

USIPOISHI NAO KWA AKILI NYINGI WATU HAWA UTAJIKUTA MATATIZONI MUDA MWINGI.

 USIPOISHI NAO KWA AKILI NYINGI WATU HAWA UTAJIKUTA MATATIZONI MUDA MWINGI.

1.Wanaojiona sahihi muda wote hawa hawachelewi kukubebesha makosa yasiyo kuhusu. 

2.Wajuaji kupitiliza hawa muda wote watakulaumu tu kwani kila jambo watakuona unakosea hata kama wao ndio wamekosea.

3.Wanaokutafuta kwenye shida tu hawa utawaona marafiki ukiwa na kitu cha kuwapa ila  siku ukiwa kwenye uhitaji watakuacha mtaroni.

4.Waropokaji hawa muda wowote watamwaga siri zako mbele ya wasiotakiwa kuzijua hivyo hakikisha hawajui mambo yako ambayo hayatakiwi kujulikana na wengi.

5 Wenye imani za kishirikina kupitiliza hawa hata kwenye jambo la kawaida wao watakushauri uende kwa mganga wa kienyeji kwa sababu wao hawaamini tena kwenye ukawaida

6.Wenye imani za dini kupitiliza, hawa pia kwenye sehemu unayotakiwa utumie akili zako wao watakushauri ufunge na kuomba ili upate majibu sasa ikiwa zaidi hii inakuwa kupoteza muda.

Pia watakushauri uvumilie hata sehemu unayotakiwa kuondoka. 

7 .Wenye wivu wa mapenzi kupitiliza, Hawa kwa muda mfupi watakufanya ufurahie mapenzi ila kwa undani zaidi watafanya ufeli mambo ya msingi kwa mfano unaweza kupata dili la maana la pesa ila watakukataza usiende kalifanya wakihofia kuibiwa kimapenzi. 

8 . Wenye mitizamo ya kimaskini, hawa muda wote wanaamini utajiri ni dhambi hivyo ukiwa nao na wakakumudu basi watakushauri uwe sawa nao.

9.Waliokata tamaa na kuridhika, hawa muda wote watakwambia maisha ndio haya haya.

10 Wenye utoto ilihali ni wakubwa, hawa watalia kwa kila changamoto yaani kwao hawana changamoto ya kuvumilia bali kulia na kukata tamaa, ukiwa nao na wakakumudu utafanana nao.

Mwanasayansi Saul kalivubha.

+255652 134707

Tuesday 19 March 2024

KOSA LIKIKUFUNZA SIO KOSA TENA BALI NI UPYA ULIOKUWA HUUJUI

KOSA LIKIKUFUNZA SIO KOSA TENA BALI NI UPYA ULIOKUWA HUUJUI.

Sifa ya makosa ni kutoa adhabu na inaweza isiwe muda huo ulipolifanya kosa ila ni lazima litakuadhibu tu mbeleni hivyo hakuna namna unaweza kukwepa adhabu ya kosa lako.

Taarifa inayopendeza ni kuwa kosa likikupa adhabu nawe ukaona kama funzo basi hilo sio kosa tena bali ni upya ambao ulikuwa huujui hapo kabla na njia pekee ya wewe kuujua huo upya imekuwa ni kupitia kukosea.

Usifanye makosa makusudi hapo utakuwa sasa unatafuta adhabu za kujitakia na yawezekana adhabu hiyo isiwe funzo lolote kwako kwa sababu sio jipya bali ulilijua kabla. 

Kwenye mchezo wa mpira timu inafungwa kupitia makosa hiivyo adhabu yake ni kufungwa magoli ila baadaye wachezaji wakimakinika kutafuta walifungwa vipi basi watagundua mbinu zipi wafanye ili wasifungwe tena  na hapo itakuwa wamejifunza kupitia makosa na adhabu waliyo adhibiwa.

Japo makosa mengine adhabu yake ni kali na utaadhibiwa tu bila  kujali hukuwa ukijua kuwa ni kosa hapo kabla ila ukimakinika zaidi utajifunza tu .Kosa bila adhabu ni ngumu kuwa funzo na kikawaida kosa lisilo na adhabu yawezekana lisiwepo labda tu uamue kutuiona hiyo adhabu.

Ukiona maisha yanakuadhibu Kwenye jambo fulani wewe kaa chini tulia utafute wapi ulikosea.


Mwanasayansi Saul kalivubha 

+255652 134707

CHANGAMOTO NI BURUDANI KATIKA MAISHA, BURUDIKA NAZO BADALA YA KULIA LIA HOVYO.

 CHANGAMOTO NI BURUDANI  KATIKA MAISHA, BURUDIKA NAZO  BADALA YA KULIA LIA HOVYO.


Mwanafalsafa mmoja aliwahi kusema ukitaka ufurahie adhabu basi ukipewa usiione kwa sura ya adhabu bali ona kama ni sehemu kama wajibu wako, kwa mfano ukipewa adhabu ya kumwagilia maua wewe ona ni wajibu wako kufanya hiyo ili maua yakue na kustawi.


Changamoto ni burudani kama zilivyo burudani ni ngumu kuburudika bila kuvuja jasho, kwenye suala la burudani kuna upande utavuja jasho na kuna upande utaburudika ila inaitwa burudani na watu hufurahi kwa sababu wameamua kumakinika na upande wa furaha kuliko upande waliovuja jasho.

Maisha ya kukosa kazi kwa muda, kuachwa kwenye mahusiano na mengine mengi yenye sura ya changamoto ni sehemu tu moja wapo  ya burudani ambayo ndio ya kuvuja jasho na kama ukiendelea kukaza utafikia ule upande wa pili wa burudani ambao ni wa kufurahia.

Kwenye hii burudani ya maisha hakuna mtu asiyepitia upande wa kuvuja jasho ambao ndio changamoto na burudani haina maana kama itakuwa na upande mmoja tu wa furaha, ukiona watu kwenye viti virefu au kokote wapo wanajipongeza basi jua wana upande mwingine waliopitia ambao ndio uliwapa hizo pesa.

Ikitokea unafukuzwa ama kukataliwa usione kwa sura ya kukomolewa au kama vile umeadhibiwa bali ona hiyo ni sehemu tu ya burudani ambapo unaandaliwa kwenda kukubalika kwingine tena panaweza kuwa pazuri zaidi ya ulipofukuzwa. Tatizo ni pale ambapo utaiona hiyo changamoto kwa sura ya kukomeshwa hapo utajikuta kwenye maumivu, kulia na kulalamika hovyo kitu ambacho hakitakupa unafuu bali kukuumiza na mbaya zaidi kukufanya uje ukosee tena kwa sababu utafanya maamuzi bila utulivu. 

Maisha yana changamoto nyingi sana na nzito ila ukisema kila moja uione kwa sura yake basi kila siku utakuwa mtu wa kulia hovyo badala ya kujifunza kupitia changamoto hizo.


Mwanasayansi Saul kalivubha

0652 134707

Saturday 9 March 2024

HARAKATI HAZIMTAKI MTU ANAYEONGOZWA KWA MIHEMKO

HARAKATI HAZITAKI MTU ANAYEONGOZWA KWA MIHEMKO.


1.Mtu ambaye akiambiwa biashara fulani inalipa anaikurupukia.

2.Ambaye akiambiwa alisemwa vibaya muda huo huo anawafuata wahusika.

3.Mtu ambaye akiambiwa kasalitiwa muda huo huo anawasha moto.

4.Mtu ambaye anataka kufanya kila kinachosifiwa sana.


KAMA UNA SIFA HIZO HAPO JUU BASI HUWEZI KUWA MWANAHARAKATI.


Kuwa mwanaharakati uwe na sifa hizi.

1.Usiyekurupuka hovyo.

2.Mchunguzi kabla ya kuongea.

3.Usiyekata tamaa kizembe.

4.Uliyetayari kukoselewa.

Michakato yote haikosi changamoto ni lazima changamoto zije kukupima kuona kweli utaweza kuyamudu mafanikio? 

Changamoto zinapokuja kuna mambo mawili ama hiyo safari sio yako au ni yako ila unatakiwa kukomaaa, sasa kabla hujasema hiyo safari sio yako ni lazima ukomae haswa maana ukiwa mtu wa kukwepa changamoto kwa sababu tu ya mihemko yako basi hakuna safari utakayoiweza hapa Duniani. 


Na ukiwa mtu wa kufanya mambo kwa kukurupukia kwa sababu tu ya mihemko yako basi utakuwa pia mtu wa kuanza upya kila mara kwani itakuwa ukifika njiani unagundua hiyo njia siyo yako bali uliikurupukia tu 


Mwanasayansi Saul kalivubha 

0652 134707

Thursday 7 March 2024

UKIONA WANAKUNG'ANG'ANIA WAKUPE UTAJIRI WA HARAKA JUA WAMEKUONA AKILI YAKO NI CHENGA

 UkIONA WANAKUNG'ANG'ANIA WAKUPE UTAJIRI WA HARAKA JUA WAMEKUONA AKILI YAKO NI CHENGA 😔 

Umewahi kusikia watu wakijinadi kutoa utajiri wa HARAKA? Yaani kulala maskini na kuamka tajiri? 

Taarifa isiyopendeza ni kuwa kama nawe ni mmoja wa wateja wao basi jua kuna kitu kwako hakipo sawa na tayari wamekiona ndio maana wanakulazimisha uingie kwenye hiyo fursa hiyo.

Wale watu wana akili sana na wapo vizuri kuisoma akili yako hasa kwenye maamuzi yako na utulivu wako na wakiona una maamuzi ya haraka yasiyo na subira basi wanajua wewe ni mteja wao mzuri katika fursa hiyo.

Tangazo lenye lengo la kutoa utajiri wa haraka huwa linawahusu watu wenye sifa hizi:

1.Wasio na utulivu, kama huna utulivu basi utakuwa mteja wao kwa sababu ukikosa utulivu utakuwa mtu wa kufanya mambo bila kufikiria kwa kina, kwa lugha rahisi unakuwa mvivu wa kupima matokeo na matendo ndio maana akija mtu akikwambia jambo fulani ukilifanya leo tu basi kesho utakuwa bilionea unaliendea kwa haraka sana bila kufikiria kuwa kama hilo jambo lingekuwepo si tungekuwa wote mabilionea.

2 Kupenda matokeo ya haraka, kama unapenda matokeo ya haraka basi nawe ni mteja kwa sababu ukiambiwa utajiri utakuja kesho haraka utaamini ila ukiambiwa utakuja baada ya miaka kumi utaona ni utapeli. Kwa lugha nyepesi hawa ni watu ambao hawana subira bali wanataka kila kianzacho leo basi kesho kilete matokeo chanya. 

3.Waliokata tamaa, mkata tamaa ni mtu ambaye haamini tena kwenye kushinda hivyo amebaki kusubiria miujiza tu , kama umekata tamaa kiwango cha mwisho basi nawe utakuwa mteja.

4.Wanaokimbizana na umri, kuna watu ambao kwa namna moja ama nyingine wanajiona kama wameachwa na umri hivyo hawataki tena kitu cha kusubiri bali wanataka tu jambo lianze leo na kesho lije na matokeo, kama upo kundi hili basi nawe ni mteja.

Matangazo haya ya kujinadi kuwa kuna utajiri wa haraka yanzidi kushia kasi kwa sababu watoaji matangazo wamegundua kuwa watu wengi sasa hivi wanataka sana mambo ya miujiza na hawataki tena kusubiria hivyo wapo tayari kulipa gharama ya kupewa utajiri wa haraka usio na uhalisia kuliko kutumia pesa hiyo kutafuta utajiri wenye uhalisia.


Mwanasayansi Saul kalivubha

+255652134707

Monday 4 March 2024

MAISHA SIO MSTARI MNYOOFU,KONA ZISIKUFANYE UTOKE MCHEZONI

 MAISHA SIO MSTARI MNYOOFU, KONA ZISIKUFANYE UTOKE MCHEZONI.

Kinachotutesa wengi ni kuishi kwa imani kuwa maisha ni mstari mnyoofu na hili sio tu tumelijenga sasa la hasha! Bali hata mifumo ya malezi inachangia hilo.

Kuna ambao wamelelewa kwa kuaminishwa kuwa vitu hupatikana kwa wakati ule watakao  hivyo kufanya ukubwani watu wapate shida sana pindi wanapokutana na uhalisia wa maisha kuwa maisha sio mstari mnyoofu.

Utotoni tuliamini kwa ambao wamefika shule wengi  waliamini shule ikiisha tu leo basi kesho wanapata ajira na wakipata ajira tu tayari wananunua nyumba, gari, kuoa/kuolewa na  kufurahia maisha. Hii nadharia ambayo inaonyesha kuwa maisha ni mstari mnyoofu lakini tukija kwenye michakato ya maisha ni wachache sana wanaopitia mstari mnyoofu na hata kama mambo yako yatakunyookea kwenye jambo moja basi kwenye jambo la pili mambo hayakuwa na unyoofu. 

Utotoni ilikuwa kila ukililia kitu unapewa kwa wakati na  hapa ndio mwanzo wa imani hiyo kuwa maisha ni mstari mnyoofu ilipoanzia ambayo ipo kinyume na uhalisia wa maisha. 

Maisha sio mstari mnyoofu na kuwa hivi haimaanishi kwamba ni changamoto bali ndio uhalisia wenyewe ambao unatakiwa kupambana nao na sio kujiona mtu mwenye mikosi kwa sababu tu umemaliza shule na kukaa mtaani miaka mitano bila kazi, umeachika kwa mchumba uliyempenda au umeanza kazi tu unataka kila kitu ununue kwa mshahara mmoja hilo haliwezekani na ukitaka liwezekane basi utajikuta gerezani. 

Kuna ambao wanaanza mahusiano yao ya kwanza na yanageuka ndoa ila kuna wengi ambao wanapitia dhoruba kadhaa za kuachika ndio baadaye zinakuja ndoa, kuna muda maisha yanakupitisha sehemu ambayo hapo zamani ulijua wanaopitia humo wana dhambi kumbe ni mapito tu kuwa maisha sio mstari mnyoofu bali kuna kona nyingi za kukomaa nazo.

Kuna wanaomaliza vyuo na kupata ajira ila kwa zama hizi kuna mtu mpaka kasahau kuwa na yeye alisoma chuo kwa sababu ana miaka mingi mtaani. Kumaliza chuo na kukosa ajira haimaanishi kuwa maisha ndio yamefikia ukomo bali hiyo ni kona ambayo unafaa ukomae nayo na hapo ndipo ujuzi wako wa udereva unapimwa.

Dereva mzuri haogopi kona za bara bara, ukiona dereva anataka tu apite barabara tambarare na kukwepa kila barabara yenye kona basi kuna shida kwenye ujuzi wake tena cheti chake kichunguzwe na vivyo hivyo hata kwenye harakati za maisha kama unataka kila jambo lako lisiwe na kona basi haya maisha yatakushinda kwa sababu kuna muda utajua kesho utapata ila unakuja kupata kesho kutwa .

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha.

+255652 134707

Sunday 3 March 2024

KAMA UNATOKA UKOO HUU BASI JUKUMU LA KUTENGENEZA UKOO MPYA TAJIRI LINAKUHUSU LA SIVYO UWE PIA MASKINI NA WEWE

 KAMA UNATOKA UKOO HUU BASI JUKUMU LA KUTENGENEZA UKOO MPYA TAJIRI LINAKUHUSU LA SIVYONAWE MASKINI. .

Dhana kuwa mambo hufuata watu ndani ya ukoo ina ukweli wake na mifano yake ipo wazi tu , tukiachana na mfanano wa vinasaba pia hata mazingira huchangia hali hiyo japo kwa ulimwengu wa kiroho watalaam wanasema kuna roho huwa zinatembea ndani ya ukoo fulani. 

Ulimwengu wa kitajiri na maskini kuna koo utakuta ni tajiri kutoka Babu mpaka mjuu na kuna koo utakuta ni maskini kuanzia Babu mpaka mjukuu na hapo ndipo kwenye dhana ya urithi wa utajiri na umaskini. 

Umewahi kuona ukoo fulani mtu mmoja tu ndio tajiri ila wengine wote ni maskini? Kama ndio Jaribu kufuatilia historia ya huyo mtu lazima katumia nguvu kubwa kuwa hivyo wa pekee na hiyo nguvu ndio inaitwa nguvu ya kujiengua kutoka kwenye ukoo maskini na kujitengenezea ukoo tajiri vivyo hivyo kuna mtu maskini ila wengi kwenye ukoo wake ni matajiri basi huyo yupo anajiengua kutoka ukoo tajiri na kutengeneza ukoo wake maskini. 

Sio kazi kubwa kujijua upo kwenye ukoo upi bali angalia tu viashiria kama kwenu hakuna tajiri na historia ya babu zako pia hali ilikuwa hivyo hivyo basi jua una kazi kubwa ya kufanya kuukana ukoo huo na kutengeneza ukoo mpya tajiri ( sina maana uukane kuwa wewe sio mwana ukoo la hasha bali uukane umaskini unaotembea kwenye ukoo wenu), Sasa uta ukana vipi?

HAYA NDIO MAMBO YA KUFANYA ILI KUACHANA NA UKOO MASKINI NA KUTENGENEZA UKOO MPYA TAJIRI. 

1.Kwenye kuoa/kuolewa jitahidi uambatane na mtu ambaye sio maskini wa fikra ( anaweza kuwa maskini wa kipato ila asiwe maskini wa fikra yaani akilini awe tajiri ajaye tena kwa vitendo).

2.Usisumbuke kumaliza umaskini wa ukoo wenu hili hutaweza bali nawe utaishia kuwa maskini pia bali anza kuandaa utajiri mpaka utakao wazaa waukute ili waanzie pale ulipoishia wewe. 

3.Kubali kulaumiwa na wana ukoo bali usiache kuwa sawa nao maana ukianza kujipata lawama zitakuwa nyingi sana na hasa pale utapokuwa ukikwepa mizigo yao kwa mfano wataanza kutaka usomeshe watoto wao wote, uwajengee nyumba na mengine mengi lakini je kweli ukiwafanyia hivyo utatoboa ?

3.Wekeza kwenye mipango ambayo hata ukifa yenyewe haifi bali itaendelea kuishi na hivi ndivyo wafanyavyo matajiri wote ambao wanataka utajiri wao usife pindi wao wakifa.

4.Usikubali kuwa mshirikina ili upate utajiri hapa nawe utakuwa maskini tu kwa sababu kwenye hizo imani za kishirikina kuna laana tupu na kuna ambao wameishia jela na hata utajiri hawajapata , kufikiria utajiri kwa njia ya kishirikina ni matokeo ya uvivu wa kufikiria na kukosa utulivu wa subira.


4.Andaa watoto wako kuwa matajiri pindi wakiwa wadogo na kwenye hili uwe mkali kidogo kwa sababu wanaweza kulemaa wakihisi hata wasipo pambana bado tu watarithi utajiri wako, waandae zaidi kuendeleza mali na sio kurithi mali .

5.Usikate tamaa kizembe ukiona harakati zinakuwa ngumu kwako usianze kujifariji kwa kauli zisizo faa na za kimaskini kama vile 

" Maisha ndio haya haya"

 "Maskini pia ni mtu"

"Sisi kwetu ndivyo tulivyo hatuwezi biashara "

Hizo ni kauli za kimaskini na zisizo na ukombozi wowote ule kifikra bali kukukandamiza tu kuwa maskini zaidi.

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

#fikia ndoto zako 

+255652 134707

Tuesday 27 February 2024

IFIKE MUDA UJANJARUKE NA WEWE KATAA KUFANYWA FURSA ISIYO NA FAIDA KWAKO

 IFIKE MUDA UJANJARUKE NA WEWE KATAA KUFANYWA FURSA ISIYO NA FAIDA KWAKO. 


1.Unakubalije kuwa na mtu ambaye kila akikutafuta basi ana shida. 

2.Unakubalije kuhusiana na mtu ambaye bila wewe kumtafuta basi mahusiano ndio yanakufa .

3.Unakubalije kuwa na rafiki ambaye anataka umtimizie mambo yake kila anapotaka la sivyo anakuchukia 

4.Unakubalije kuwa mtu wa kuonewa hovyo hovyo?


WATU WA HOVYO WANAWEZA KUWA KIKWAZO KWAKO KUFANIKIWA. 


Kuna watu lazima ufanye tu maamuzi magumu ya kuwaepuka na hapo ndipo utagundua kuwa walikuchelewesha kwa sababu utaanza kuona matokeo chanya kwako.


Taarifa isiyopendeza ni kuwa kuna watu wamekusoma vya kutosha na wamekuona hujielewi hivyo wanakutumia kama mtatuzi wa shida zao huku wewe ukiendelea kuangamia taratibu. 


Kila siku jifunze kuhusu watu bila kusahau kuwatathimini marafiki zako ili ujue nani yupo kwako kweli na nani yupo kwako kukutumia hovyo. 


Mwanasayansi Saul kalivubha

Fikia Ndoto zako 

+255652 134707

Sunday 18 February 2024

KAMA LENGO LAKO KUU NI KUZAA ILI WATOTO WAJE KUKULIPA FADHILA KWA MALEZI BASI NAKUSHAURI HAIRISHA KUWA MZAZI KWA SABABU WEWE NI MJASIRIAMALI NA SIO MZAZI.

 KAMA LENGO LAKO KUU NI KUZAA ILI WATOTO WAJE KUKULIPA FADHILA KWA MALEZI BASI  NAKUSHAURI HAIRISHA KUWA MZAZI KWA SABABU WEWE NI MJASIRIAMALI NA SIO MZAZI.

Ni ushauri tu sio lazima ufuatwe na wote ila unaweza kuutafakari kabla ya kuupinga kwa mihemko ya hoja zisizo na mashiko.Kama hujui kwanini tunazaliana sio vibaya ukapitia upya tena hata maandiko ya Mungu ili uone hata huko lengo kuu halisemi  kuzaa ili watoto waje kukulipa fadhila kwa malezi yako na kama hapo bado haitoshi basi Jaribu kukaa na wazee hasa wenye umri wa miaka sitini utasikia wengi wao wakilalamika kuwa watoto wao hawawasaidii ila usikomee hapo nenda kafuatilie maisha ya hao wanaopewa lawama utakuta maisha yao bado pia yanahitaji utegemezi yaani bado hata wao hawajajimudu sasa swali ni je ni sawa kulaumiwa?

Kama sio changamoto mfano kubakwa na kusababishiwa ujauzito basi usikurupuke kuwa mzazi ilihali hujajua kwanini unatakiwa kufanya hivyo.


Usiwe  mzazi kwa ulimbukeni tu  bali jiulize upo tayari kulipa gharama za kuwa mzazi? Au ndio unataka uwe yule mzazi ambaye anatoa malezi kwa mkopo ili baadaye alipwe?

Kuna watoto hawasemi tu ila ukweli wanashindwa kuwaelewa wazazi wao kwa sababu mpaka wanatamkiwa maneno ya laana kwa sababu tu hawataki kuwalipa fadhila wazazi wao , wazazi wamekuwa wakiwatamkia maneno makali na kusema bila aibu kuwa waliuza sijui nyumba ili watoto wasome sasa huo ni wajibu wa mzazi kumuandaa mtoto ikiwemo kumpa elimu sio uje kumdai baadaye naye akulipe.

Mzazi jiandaye vizuri kabla ya kuwa Baba au mama na elewa kuwa utatakiwa kuwajibika kimalezi bila kufikiria kulipwa fadhila.

Watoto wengi wamekuwa wanaishi kwa kukosa utulivu kwa sababu wanalazimishwa kuwajengea wazazi nyumba bila hivyo wanatishiwa kupewa laana sasa Kama umri wako wote wa ujana umeshindwa kujenga na tena usikute ni kwa uzembe wako tu iweje uwabane watoto wakufanyie hivyo na kibaya zaidi unakuta ndio kwanza mtoto kapata ajira au ndio kwanza anajitafuta ila tayari mezani umemlundikia matatizo yote ambayo wewe ukiwa na nguvu yalikushinda.

Kushindwa kujiandaa kwako mzazi ni chanzo cha matatizo kwenye familia za watoto wako kwa sababu mtoto ataogopa mpaka kuoa kwa sababu tu akijiongezea majukumu atashindwa kukuhudumia wewe na kwa wale ambao watalazimisha kufanya hivyo basi itazuka vita kati ya mzazi na mkwe wake kwa sababu mzazi ataamini hajaliwi kwa sababu mkwe ameingilia kati.Kwa mtoto wa kike naye ndio pale analazimishwa kuolewa na mtu mwenye pesa tu ili awe Kama kitega uchumi na kama sio hivyo basi ndio akiolewa anabanwa awe anatuma pesa mara nyingi mwisho wa siku mumewe anagundua hivyo tayari ndoa inaanza migogoro na yote hayo ni kosa tu la mzazi Kushindwa kujiandaa kujitegemea na kutaka watoto wamlipe fadhila.


Mzazi tambua kuwa kumtunza mtoto ni wajibu wako sio kumkopesha na jukumu la kujitunza wewe ni lako japo watoto wanaweza kukusaidia ila sio kitu cha kutegemea kwa sababu na wao wana majukumu ya kuanzisha familia na kujitafuta pia kiuchumi ili uzao uendelee, ukizeeka au ukawa unaumwa na huwezi kujimudu basi hapo watoto watachukua jukumu la kukutunza ila bado una nguvu na sio mzee unaanza kuwabana watoto wakulipe fadhila je wakaibe ? 

Kushindwa kujiandaa kwa mzazi ndio mwanzo wa kulaumiana kwenye familia mpaka ukoo na hii ni pale ambapo watoto wako mwenyewe unataka ndugu wakusomeshee na wakisema hawawezi tayari unawatupia lawama nyingi  tena bila aibu unaongea hata mbele za watu kuwa kina fulani hawataki kusomesha watoto zako ilihali wana pesa bila kufikiria kuwa na wao wana mizigo yao pia hata kama wana pesa ila unajua bajeti zao? Kilichofanya yote hayo ni wewe hapo kwanini lawama wapewe wengine?

Mzazi kamili hujiandaa yeye na kuwaandalia watoto pia na kwa kufanya hivi ni rahisi kuvunja mnyororo wa umaskini kwa watoto wakizaliwa wanajipambania  wao na wajukuu zao na sio tena uwape familia nyingine yaani wapambane kwa ajili ya watoto wao na huku pia wakupambanie wewe. 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

+255652 134707

Saturday 10 February 2024

KAMA HIVI NDIVYO UNAVYOISHI MJINI NI BORA URUDI TU KIJIJINI UKAISHI KULINGANA NA KIPATO CHAKO

 KAMA HIVI NDIVYO UNAVYOISHI MJINI NI BORA URUDI TU KIJIJINI UKAISHI KULINGANA NA KIPATO CHAKO.

Yawezekana hii isiwe makala nzuri kwa waishiyo mijini huku wakijisifu kila siku na kuwabeza waishiyo vijijini ila ukimakinika na kuchukulia chanya basi kuna jambo utajifunza. Kuishi mjini ni ndoto ya wengi nafikiri inaweza kuwa zaidi ya asilimia hamsini ya watu wanatamani kuishi mjini na hasa kwenye miji ile mikubwa  lakini uhalisia ukoje huko mjini kwa wengi wao? Kuwa kwenye changamoto  mjini sio sababu pekee ya kusema uhame urudi kijijini/mkoani la hasha ! Hapa namaanisha kwa wale ambo mjini hawapawezi kabisa ila wanapang'ang'ania  tu kwa sababu zisizo na msingi.

Bila shaka utakuwa umewahi sikia ama kuona baadhi ya watu waishio mijini wakiwabeza watu waishio vijijini ama mikoani kama wasemavyo watu  wa Dar es salaam na kibaya zaidi hudiliki kusema watu wa vijijini ni washamba na wasio wabunifu wa maisha, Sio uongo kuwa kuishi mjini kunakomaza akili kulinganisha na kuishi kijijini kutokana na harakati kuwa nyingi mjini na panahitaji wepesi sana katika maamuzi ili uweze kumudu mjini lakini kwenye maamuzi hayo hayo kuna watu wapo mijini kuongeza idadi tu ya watu ila ki uhalisia wanaishi maisha magumu sana kwa lugha isiyo rasmi ni kuwa walikurupuka kuja mjini ilihali hawana mipango ya kuwafanya wanufaike na maisha ya mjini. 

Ikiwa unaishi mjini kwa sababu moja wapo kama  nimevyoelezea hapa chini  basi haraka toka mjini urudi mkoani/kijijini  ama jitafakari zaidi ubadili mtindo wako wa maisha.

Kuishi mjini ki ulimbukeni; Unaishi mjini kutaka tu uonekane nawe unaishi mjini yaani ukisimama na kujitambulisha ama kutambuliswa unaishi mjini hiyo ndiyo furaha yako kuu bila kujali hali ngumu unayokutana nayo huko mjini na kama hii ndio sababu pekee ya wewe kuishi mjini basi haraka ondoka mjini kwa sababu unaongeza tu idadi ya watu na usipokuwa makini maisha yatakuchapa  na kujikuta kwenye hali mbaya kimaisha mpaka kwa uzao wako pia, kwa sababu utatumia gharama kubwa kuwafanya watu wajue kuwa unaishi mjini ilihali hiyo gharama ungeitumia kuboresha maisha yako huko mjini, kila siku utakuwa mtu wa kuchapisha maudhui mitandaoni ya kukuonyesha upo mjini ambapo vocha zitateketea tu bure na hakuna unachokiingiza tofauti na sifa ambazo hazikuingizii pesa. 

Kuishi mjini kwa sababu umepazoea; Kuna mtu maisha ya mjini kwake ni magumu sana na kikawaida tayari yamemshinda ila  ukimpa fursa za kurudi mikoani/kijijini anaweza hata kukutukana na ukitaka kujua sababu anakwambia kapozea mjini hivyo itampa sana tabu kuanza tena upya huko mikoani  kama wewe ndio huyu jua kabisa mjini hapakufai ondoka haraka la sivyo jiandaye kuzeeka maskini.

Kuendelea kuishi mjini kwa maisha magumu ukiogopa kuchekwa endapo utarudi mkoani/kijijini; Huyu pia hafai kuishi mjini kwa sababu hatofautiani sana na mtu limbukeni na asiye na malengo,Huyu yupo tayari kufanya maamuzi ila anaogopa macho ya watu ilihali mjini pememshinda  kuishi sasa nawe jiandaye kuishi maisha magumu sana kwa sababu huna mbinu za kutatua changamoto ili umudu maisha ya mjini bali upo tu kuonekana mtoto wa mjini ilihali maisha yamekushinda .

Kuishi mjini huku unategemea mshahara tu kama chanzo pekee cha pesa na huna chachu yoyote ya kuongeza vyanzo vingine vya pesa; Hili kundi lina watu wengi sana na hapa ndipo utakuta mtu anaishi mjini kimateso sana na hana mpango wowote wa kujinasua na mateso hayo , Kwa mfano unategemea mshahara tu ndio ulipe kodi ya nyumba,ukupe  nauli zako za  kila siku kukupeleka kazini, ukupe ada ya watoto tena shule za mjini hawana huruma kama huna ada mtoto watamfukuza tu sasa hapo kweli utaishi maisha ya furaha? Sio kwamba kila siku utakuwa mtu wa kulalamika tu kwanini mishahara haipandi . Kama wewe ndio huyu ondoka haraka mjini urudi mkoani kwenye nyumba nzima unapanga elfu hamsini na bado zipo jirani na unapofanyia kazi hivyo  huna haja ya kulipa nauli , haya kwako yatakuwa maamuzi sahihi kwa sababu huko mjini pia umekaa tu hutaki biashara hivyo ni bora urudi kuishi kwa kutegemea mshahara sehemu yenye maisha rahisi. 

Kama unaishi mjini huku ukisifia tu maisha mazuri ya mjini na jinsi watu walivyo na majumba makubwa na magari ila wewe huna hiyo nyumba na wala gari pia ; kama wewe pia ni huyu basi  mjini hapakufai tena ondoka haraka kwa sababu upo kwenye kundi lisilo lako na mwisho wa siku shida utapata wewe, upo mjini kushangaa tu wengine wakifanya maendeleo ila wewe unaendelea kuwa mteja wao kwa  kuwaongezea kipato tu sasa unafanya nini mjini? 


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

+255652 134707 

Saturday 3 February 2024

MAMBO UNAYOTAKIWA UFANYE UKIWA NA UMRI KATI YA MIAKA 20 MPAKA 30

 KIJANA JITAHIDI USIJIPOTEZE UKIWA NA UMRI KATI YA MIAKA 20-30

Katika makuzi kuna mgawanyo wa hatua takribani nne ambapo karibu kila mtu kwa kudra za mwenyezi Mungu huzipitia, Vipindi hivyo hugawanywa kwa kuzingatia umri na matukio yake na pia kila kipindi ni muhimu zaidi katika kuandaa kipindi kingine hivyo kumbe hutegemeana.Japo hatua hizo za makuzi hutegemeana ila ipo hatua yenye changamoto nyingi na iliyomuhimu sana na mtu usipokuwa makini utajikuta unajipoteza na ukiwa makini zaidi utajipata .

UMRI KATI YA MWAKA 1 MPAKA MIAKA 18 , Huu ni umri wa kujidanganya sana na kutengeneza malengo ya ukubwani  na kwanini kujidanganya? Kwa sababu unakuwa unaona kila kitu kitawezekana bila kusubiriwa kwa mfano: Utaona utamaliza shule mpaka chuo na baada ya kumaliza tu utapata kazi ya kuajiriwa na pengine ukipata kazi tu utalipa fadhila kwa waliokusomesha /kukusaidia na kisha utaoa/kuolewa na ndani ya mwaka huo huo utapata mtoto wako wa kwanza. Hivi ndivyo wengi tulipanga tukiwa na umri huo na walio kwenye umri huo pia wapo wanapanga wakiamini maisha ni mstari mnyoofu hivyo kila kitu kitaenda bila shaka yoyote, Je ni vibaya kupanga? Sio vibaya ndio maana awali nikatangulia kusema kuwa huu ndio umri wa kujiona ukiwa mkubwa utakuaje, Kwanini ni umri wa kujidanganya? Tuone hatua ya pili kisha hili jibu litapatikana.

UMRI KATI YA MIAKA 20- 30 ( UMRI WA UHALISIA) Huu ndio umri wa kuona vitu kwa vitendo kwa namna kijana alivyojichora akiwa na miaka 18 kurudi nyuma,Kwenye umri huu ndio utaona maisha ni mstari mnyoofu ama ni mstari wenye kona nyingi? Katika umri huu kwa wale ambao walienda shule wengi humaliza elimu zao mpaka za vyuoni na kikawaida ndipo wanakaribishwa rasmi mtaani na hapa ndipo uhalisia unaonekana.

Katika umri huu mambo mengi yanakuja kinyume na namna mtu alivyofikiri japo yanatimia ila kuna kitu kinaitwa Subira ndio hasa kinafaa kitumike kwenye umri huo kwa sababu ukiwa mtu wa pupa lazima utakata tamaa na kuona maisha ni magumu sana.

Sio ajabu kumaliza shule ukajikuta unapata kazi baada ya miaka mitano tofauti na ulivyojiona kuwa utamaliza leo na kesho utaitwa kazini.

Sio ajabu ukaoa/ kuolewa nje umri uliojipangia kwa mfano ulijua utamaliza tu chuo utaingia kwenye familia ila unamaliza unakaa tena miaka mitano mbele ndio unaanza familia. 

Sio ajabu ukaingia kwenye familia mapema tu ila ukakutana na  changamoto za uzazi ukajikuta unapata mtoto wa kwanza baada ya miaka 7 ya ndoa tofauti na ulivyoona ukiingia tu leo kwenye ndoa basi kesho tayari mimba na hata usijaliwe kupata maana yote ni mipango ya Mungu.

Sio ajabu ukavuka miaka 20 bila kuwa na kiwanja wala nyumba ukiwa bado umepanga au hata kuishi kwa wazazi  tofauti na ulivyojiona kumiliki nyumba na usafiri ukiwa kati ya  miaka 20 tu.

Hayo ni baadhi ya matukio ambayo yapo na wengi huyapitia na ndio inakuja ile sababu ya huu umri kuitwa umri wa UHALISIA, na huu umri unatufundisha kuwa maisha sio mstari mnyoofu na kutokuwa mstari mnyoofu haimaanishi kuwa malengo hayawezekani la hasha bali subira inatakiwa sana katika umri huo la sivyo utajipoteza kwa kuwa mtu mwenye haraka na mwisho wa siku unaishi maisha yasiyo ya uhalisia wako kwa mfano ulihisi utapata nyumba na gari haraka sasa ili kutaka yawezekana unaingia kwenye wizi au kwa waganga wa kienyeji wanakwambia utoe kafala mwisho wa siku unaishia gerezani .

Umri huu hutakiwi kuwa na haraka bali kuwa na juhudi tu za kupambania ndoto zako na sio lazima zije kwenye mstari mnyoofu ila ikitokea zinakuja kwenye unyoofu basi shukuru Mungu kwa hilo maana upo kwenye kundi la wachache ambao mambo yao yanakuwa kwenye unyoofu pasi na chenga.Usikubali ujipoteze hapa kwa sababu ukijipoteza kuna uwezekano mkubwa nyakati zitazofuata zisikusaidie kujipata tena.

UMRI KATI YA MIAKA 40- 55, Huu ni umri wenye matukio mawili makubwa la kwanza ni kukubali matokeo  huku ukilazimisha uendelee kuonekana kijana wa miaka 30 ,hii ni wale ambao walikata tamaa na kuona maisha ndio haya haya hivyo wanaamua kuridhika lakini changamoto nyingine inayowakabiri ni kupingana na umri yaani hawataki kukubali kuwa wao ni watu wazima na utajigundua hivyo pale ukianza kuona  unalazimisha kufanya vitu visivyo endana na umri wako, kitaalamu hiki kipindi kinaitwa mid age crisis(kuupinga utu uzima)

Tukio la pili ni wale ambao hawakukata tamaa hivyo wanaendelea kujitafuta na uwezekano wa kujipata upo  .

Changamoto kubwa kwenye umri huu ni kuwa majukumu yanakuwa mengi sana hivyo utegemezi unakuwa mkubwa hivyo kama hukujipanga vizuri utakuwa unapata pesa ila zinaishia kwa wategemezi wako.

UMRI KUANZIA MIAKA 60 KUENDELEA, Hapa ni uzee tu na kupumzika ijapo bado kuna wengine wataendelea na kutafuta tu kama matokeo ya kushindwa kutumia ujana wao vyema au kushindwa kuweka mikakati mizuri ujanani. 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

+255652 134707

Friday 2 February 2024

JIFUNZE KUTOFAUTISHA WATU HAWA WAWILI WANAOKUJA KWAKO KIMAHUSIANO

 JIFUNZE KUTOFAUTISHA   WATU HAWA WAWILI WANAOKUJA KWAKO KIMAHUSIANO.

Karibu tena ndugu msomaji kwenye blogu hii ya fikia ndoto zako kwa minajiri ya kuongeza maarifa, leo tutazame kidogo kuhusu aina hizi mbili za watu wanaokuja kwako kwenye mahusiano. 

Mahusiano sio kitu kigeni na hasa mahusiano ya kimapenzi yamekuwa yakiimbwa kwa ubaya na uzuri kila uitwao leo, kwenye hii Dunia kila mtu ni lazima ahusiane kama hutofanya hivyo kwenye mahusiano ya kimapenzi basi utafanya hivyo kwenye mahusiano ya kijamii hivyo hakuna namna unaweza kukwepa kuhusiana.

Kwenye mahusiano kuna kufaana na kushindwana ndio maana kila siku tunashuhudia matukio makubwa mawili ambayo ni watu kuendelea kuhusiana na huku wengine wakiafiana kuachana, Kwenye kuendelea kuhusiana haimaanishi kuwa wameendana kwa sababu kuna wengine wafanya hivyo kwa sababu tu wanajiona wamekosa pakwenda na kwenye kuachana yawezekana mnaendana ila mmoja tu kushindwa kuwa na subira ama kushindwa kujifunza kuishi na mwenziwe. 

Kuna makundi makubwa mawili ya watu ambao wanakuja/watakuja kwako kimahusiano hivyo ukiyafahamu hutopata shida ya kukabiliana na matokeo ya kila kundi.

Kundi la kwanza ni yule MTU ANAYEKUJA KUKUANGALIA KWELI WEWE NDIYE?

Huyo ni yule ambaye hajui nani anamtafuta hivyo atakuja kwako kama kubahatisha tu ukiwa ndiye atakaa na ukiwa siye ataondoka, hili ni kundi lenye watu wengi sana na kwa ufupi mimi huwa naliita kundi ambalo linajifuta kwenye mahusiano yaani bado wanachama wake hawajui kipi wanataka hivyo wanapoingia kwenye mahusiano wanakuwa mguu mmoja nje na mwingine ndani, utalitambuaje kundi hili? Huwa wana sifa zao zinazo fanana  kwa kiwango kikubwa.

TABIA YA WANAKIKUNDI HIKI NI KAMA ZIFUATAZO:

1.Wanakuwa kama waamuzi wa mpira tu muda mwingi wanatafuta makosa yako.

2.Hawana subira hivyo changamoto inayohitaji utatuzi wa pamoja wao ndio wanaichukulia kama mlango wa kutokea.

3.Hawasamii lengo moja ipasavyo hasa la kwanini wanahusiana yaani ukimuuliza kuhusu kesho yenu kwenye suala la pamoja anakuwa na maelezo mengi yanayokingana yenyewe, wapo hivi kwa sababu wanakuwa hawana uhakika kweli wewe ndiye?

4.Huwa hawatulii na mtu mmoja kwa sababu hawajui nani wanamtafuta hivyo hujikuta kwenye mahusiano na watu wengi 

5.Muda mwingi wanakuwa kama wapelelezi.

6.Kuachana kwao sio jambo dogo na muda mwingi watatishia hivyo hasa changamoto inapojitokeza.

7.Hawapendi kutafuta suluhisho bali wanakuwa kishari zaidi pindi amani inapotakiwa.

8.Wanakuwa na haraka sana na utalijua hilo kwa kuona wanataka mambo yawezekane bila kughairishwa kwa mfano mmepanga kukutana na bahati mbaya ukakutwa na changamoto na ukatoa taarifa ila kwake anaweza kutumia changamoto hiyo kama fimbo ya kukuadhibu na mkaachana.


Kundi la pili katika eneo hili ni MTU AMBAYE ANAKUJA KWAKO KUKAA.

Huyo anajua nani anamtafuta hivyo haji kwako kwa kubahatisha bali kajiridhisha kabla hajaja kwa lugha nyepesi hawa ni wale ambao hawapo kwenye majaribio labda wakukute wewe ndio upo kwenye majaribio uwakimbize ila ukiwa nawe upo tayari basi watajenga kibanda kwako na maisha yataendelea.

Hili ni kundi lenye wanachama wachache kwa sababu ili uwe mwanachama sifa ya kwanza lazima ujitambue vilivyo na ujue nani unamtaka.  Hili kundi ndio linafanya watu wasifie mahusiano na kuyaimba kwa uzuri wake , wanachama wake wana tabia zinazofanana na sio tabia nyingi hata.

SIFA ZA WANACHAMA WA KUNDI HILI.

1.Hawana mambo mengi hivyo wakija kwako hawaji kama waamuzi wa mpira bali wanakuja kujifunza kuishi na wewe na kufundishana pale mnapopishana.

2.Ni kundi ambalo halifichi lengo lao kuu na kupitia matendo utawaona hivyo pia.

3.Ni watafuta suluhu kwenye changamoto sio wepesi wa kutishia muachane.

Hizo ndio sifa za kila kundi na mpaka kufikia hapo natumai umejitambua upo kundi gani ama una uhusiana na mtu wa kundi gani , ikiwa upo kwenye kundi la kwanza ni bora uachane na mahusiano kwanza na uwekeze nguvu kubwa kwenye kujitafuta ili ujue nani hasa unamtafuta.

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

#fikia ndoto zako

+255652 134707

Friday 26 January 2024

WANAVYUO TUSIISHI KAMA HATUTAHITIMU

 WANAVYUO TUSIISHI KAMA HATUTAHITIMU. 

Habari ndugu msomaji wa gazeti letu pendwa na karibu tena katika safu hii , leo tuangazie wasomi wa vyuo na hasa vyuo vikuu na hatima za maisha yao mtaani( baada ya kuhitimu)

Zama zimebadilika sana kiasi kwamba muhitimu wa chuo wa sasa ni kawaida kukaa nyumbani zaidi ya mwaka akisubiria ajira ambapo kipindi cha miaka kadhaa ya nyuma muhitimu alimaliza na kupitiliza kwenye ajira , ajira ilikuwa ni uhakika tofauti na sasa ajira imebaki ni bahati.Mabadiliko hayo ni ya kawaida sana sio Tanzania tu hata nchi za wenzetu huko ulaya dimbwi la wanachuo kukosa ajira linaongezeka kila siku tukiachana na tekinolojia kuchukua nafasi za ajira zetu mfano mgunduzi wa robot unachukua nafasi ya mtu kutenda kazi lakini pia idadi ya wasomi inazidi kuongezeka sana tofauti na zama zile unakuta mtaa mzima mwana chuo ni mmoja mtaani sasa mtaa mzima kuna zaidi ya wanavyuo ishirini na zaidi. 

Nimekuwa mwanafunzi wa chuo kikuu cha afya na sayansi shirikishi muhimbili kwa miaka yangu kuishi pale kama mwanafunzi kuna jambo muhimu nilijifunza pengine kwa uliyehitimu tayari linaweza lisikusaidie tena lakini kwa aliye mwanafunzi sasa likamsaidia kwa kusoma makala hii au wewe kuwa balozi wa kufikisha ujumbe kwa anaye husika na umfundishe. 

Kumaliza chuo sio tukio la dharura ni wazi kuwa unaenda chuo leo na baada ya miaka kadhaa utarudi tena mtaani kuendelea na maisha mengine kwa kuitumia elimu yako kukupa pesa ili maisha ya kawaida yaendelee sasa utaishije?.

Ishi kama utahitimu chuo, vyuoni kuna makundi yanayonufaika na mikopo ya serikali yaweza kuwa mkopo ukawa wa 100% au pungufu ya asilimia hizo lakini bado ni mkopo hivyo lazima utaulipa tu sasa unautumiaje mkopo huo kumudu maisha yako ya chuo na kubaki na ziada kwa ajili ya kuendeshea maisha baada ya chuo?. Kuishi maisha chini ya kipato chako hii ni mbinu bora zaidi katika kuijali kesho yako , sio wanavyuo wote lakini wapo wanavyuo maisha yao ni kama tayari wamehitimu na wana kazi zao au wanaishi kama ule mkopo ni bure na wana uhakika kuwa siku wanamaliza tu na ajira watapata hivyo kuanzia utaratibu wa chakula chao, mapambo ya vyumba vyao na uvaaji wao ni gharama kubwa sana kulinganisha na mkopo wanaopewa na muda mwingine hujikuta wakiwa kwenye madeni ya kutosha tu kabla ya kupokea bumu jingine kwa mfumo huo si hata nauli ya kukurudisha kijijini baada ya kuhitimu utaikosa? 

Baada ya kuhitimu kuna maisha kabla ya kupata ajira na maisha hayo tukiachana na kula na kuvaa pamoja na sehemu ya kulala pia kuna kupeleka barua za maombi katika ofisi husika au kuzituma kwa njia ya barua pepe bila kusahau gharama za kwenda pale ulipoitwa mahojiano ( interview) na maisha yote hayo yanahitaji pesa sasa ikiwa una mkopo chuoni achana na imani kuwa pesa haitoshi wewe simamia na kufanya mambo chini ya pesa unayopewa angalia utunze hata elfu hamsini kwa kila ingizo ( bumu) hapo ukimaliza utakuwa na ziada ya kukusukuma kutafuta ajira au namna nyingine ya maisha, jiulize ikiwa utamaliza chuo na ukapata kazi sawa na ingizo la mkopo kwa mwezi maisha yatakushinda? kuna wafanyakazi mnalipwa nao thamani sawa ya pesa lakini maisha yanaendelea na ziada wanabaki nayo kwa nini ushindwe? Chunguza maisha yako kwa siku unaishi kwa gharama za zaidi ya elfu nane miatano? ( ingizo la mkopo kwa siku) jibane sana uishi hata kwa elfu tano basi ili ubaki na elfu tatu miatano itakusaidia hiyo siku ukimaliza mafunzo. 

Kuna fursa kubwa sana ambayo kwa sasa ndio ina nafasi kubwa sana katika kusaidia watu kupata ajira nayo hiyo ni kujitolea, sasa watu wanaojitolea wengi wao ndio huingizwa kwenye mfumo wa ajira iwe taasisi binafsi au za kiserikali na pia katika kujitolea kuna uzoefu unapata katika taaluma yako lakini usisahau kuwa maana halisi ya kujitolea ni kufanya kazi bila malipo ya kifedha sasa utaweza kweli kujitolea ? Kwa namna yoyote ile ukiweza jitahidi utoke chuo ukiwa na pesa ya kukufanya uishi mtaani kwa miezi sita hivyo hata ukipata pa kujitolea nina amini ndani ya miezi sita watakuwa wameshakufikiria kukulipa ndio maana nimesema angalau utoke na ziada ya miezi sita, tumia mkopo wako kwa nidhamu huku ukiishi maisha ya maandalizi. 

Makala hii imeandikwa na Saul Kalivubha , Mwanasayansi. 

+255652 134707