Tuesday, 25 August 2026

NAJUTA KUMPELELEZA MCHUMBA WANGU FACEBOOK 1

 

SEHEMU YA KWANZA “NAPOKEA FRIEND REQUEST”

Ilikuwa Jumapili nikiwa nimetoka ibadani nimetulia tu kitandani kusaka utulivu wa nafsi, masaa sikuwa nayakumbuka vizuri ila nachokumbuka tu ni kwamba nilikuwa kitandani nimejilaza ili nipumzike, katika kupumzika akili ikaniambia, "Peruza kidogo mitandaoni upate starehe."

Nikaanza na na Facebook, Bila kufikiria sana nikaona ombi la urafiki mpya Jina lilikuwa Koku Muganizi. Sikufanya upekuzi wowote kwa sababu ilikuwa si jambo jipya kukubali maombi kama yale hivyo haraka tu nikaibonyeza "kubali" na kuendelea na maisha yangu.

Baada ya dakika chache alama ya meseji ikaonekana, nilipoingia nilikuta jumbe 3 kutoka kwa huyo rafiki mpya:

"Mambo"

"Asante kunikubalia urafiki"

"Nimefurahi kuwa sehemu yako"

Kama mwanaume, ukipata ujumbe kutoka kwa jinsia ya kike moyo unakuwa mwepesi hivyo bila ajizi niliingia haraka kwenye profile yake nikakuta picha tatu tu za binti mtulivu, mstaarabu na mzuri.

Tukaanza kuzungumza kidogo kidogo lakini kitu kimoja kilinisumbua kichwani nacho ni jina lake halikunipa uhakika kwamba ni msichana kweli maana zama za leo utapeli ni mwingi sana hivyo nikaamua kumpima kwa utani ili kuthibitisha 

Mimi: "Yaonekana wewe ni msichana mtulivu sana" 

Yeye: "Kawaida tu hata wewe pia ni kijana mtulivu."

Jibu lake lilikuwa la haraka sana likafanya nikose la kusema zaidi.

Niliamka kwenda chooni, niliporudi nilishangaa kupata meseji yake kwenye WhatsApp na ilikuwa ni yeye yule yule wa Facebook, Moyoni nilisema, "Labda kachukua namba yangu mahali."Lakini kilichonifanya nisimame ni kitu kingine. Alikuwa ananiita kwa majina yangu yote matatu ya kuzaliwa.  Tatizo ni kwamba Facebook yangu ina majina mawili tu hilo la tatu nililificha, Sasa alilijulia wapi?

Sikumuuliza bali niliijaribu kujipa majibu yangu mwenyewe. "Labda Facebook inaongeza kiotomatiki."

 

Tulizidi kuwasliana mpaka kupeana historia zetu na hapo ndipo tukagundua kuwa tunatoka mkoa mmoja ingawa wilaya zetu ni tofauti yeye alikuwa Bukoba na mimi Muleba, Unajua furaha ya kukutana na mtu wa nyumbani nje ya nyumbani? Inaleta utamu tofauti kabisa.

Siku chache tu, tulikuwa tayari tumeshaingia kwenye mahusiano na wote tulikuwa w mbali na nyumbani, yeye kikazi na mimi pia lakini alinihakikishia kitu kimoja kuwa atakapokuwa na nafasi nitapita kukusalimia maana wote tulikuwa Dar es salaam. Maneno hayo kwa mwanaume ni kama mafuta kwenye moto hakuana asiyependa kutembelewa na msichana.

Siku moja akaniuliza: 

"Unajua tarehe 12 Mwezi wa Sita ni siku yangu ya kumbukizi kuzaliwa?"

Nilijibu kwa furaha: "Nitakutumia kitu hata kama ni zawadi ndogo na kama tutaonana tutasheherekea pamoja" 

Akanijibu: "HAPANA SHAKA. KUNA SIKU ITATUKUTA PAMOJA." Japo tulikuwa pamoja Dar ila sikutaka kuonekana ninaharakisha sana kuoanana naye, Japo ndani yangu kulikuwa na swali moja linaninyima usingizi: Alipata wapi namba yangu? Na alijua vipi jina langu la tatu?

Nikaamua kufanya upelelezi wangu mdogo, nikaangalia kama tunachangia marafiki na kweli, nilimkuta ana rafiki mmoja tuliyesomea naye hapo moyo ukatulia kidogo. Lakini kabla sijapumua, akanitumia ujumbe: 

"Mbona unaonekana una hofu?"            

Nikajibu: "Sina hofu." 

Akarudi tena: "Nafahamu una hofu ya wapi nimepata mawasiliano yako ni rafiki zako. Ndio wamenipa namba yako na majina yako yote."

Damu yangu iliganda, kafahamu vipi kuwa nilikuwa na hofu? Nikaamua kuwapigia wale marafiki zangu na wote walinipa jibu moja:  "Tunamjua tu Facebook ila hatujawahi kuzungumza naye" Nikiwa bado kwenye mshtuko huo, ndipo ujumbe wake mpya ukaingia:  "Wale rafiki niliokwambia sio hawa wa Facebook."

Hapo ndipo hofu yangu ilipanda kilele, Huyu mtu ni nani? Nilijaribu kujituliza. "Labda ni mtu tu aliyenifahamu barabarani akampa taarifa zangu."

Tarehe 12 Juni ilifika ambayo ni siku ya kumbukumbu yake ya kuzaliwa na asubuhi nilimtumia ujumbe wa kumpongeza na kumuahidi kumtumia pesa anunue hata soda., Alifurahi. Baadaye mchana Facebook ilinijulisha: "Leo ni siku ya kuzaliwa kwa Koku Muganizi."  Niliingia kwenye ukurasa wake na picha yake ilikuwa nzuri sana hata kwenye sehemu ya maoni watu wengi walikuwa wakimiminika kumtakia heri ya kuzaliwa japo sikufanikiwa kusoma ila niliamini hivyo. Nilijaribu kusoma sasa maoni lakini hayakufunguka, Nikajaribu kuandika yangu ya kumtakia heri nayo yakakataa nikasema, "Labda ni mtandao."

Akanitumia ujumbe: "Leo Facebook yangu haiko sawa." 

Nami nikakubaliana naye lakini akaniambia, "Jaribu tena."

Niliporudi, mwisho maoni yalifunguka nikapiga hatua kuteremka ili nione ni nani kamtakia heri. niliwaza, kama ana mchumba lazima nimpate hapa kisha nikakutana na maoni ambayo yalibadilisha kila kitu kwenye fikra zangu kwanza maoni mengi yalikuwa kwa lugha nisiyoelewa. labda ni lugha ya kwao, nikajidanganya pili nikaona lipo moja kwa Kiswahili hapo Roho yangu ikatetemeka.

Lilisomeka hivi: 

"Vipi mbona msimu huu umetucheleweshea Damu?"

Naye akajibu: 

"Punde tu mtapata. Si mnajua ugumu ulivyo sasa kuipata?"

Damu?

 Malenga wa Kiha

 Mwanasayansi Saul Kalivubha

 255652134707

1 comment: