Sunday, 18 February 2024

KAMA LENGO LAKO KUU NI KUZAA ILI WATOTO WAJE KUKULIPA FADHILA KWA MALEZI BASI NAKUSHAURI HAIRISHA KUWA MZAZI KWA SABABU WEWE NI MJASIRIAMALI NA SIO MZAZI.

 KAMA LENGO LAKO KUU NI KUZAA ILI WATOTO WAJE KUKULIPA FADHILA KWA MALEZI BASI  NAKUSHAURI HAIRISHA KUWA MZAZI KWA SABABU WEWE NI MJASIRIAMALI NA SIO MZAZI.

Ni ushauri tu sio lazima ufuatwe na wote ila unaweza kuutafakari kabla ya kuupinga kwa mihemko ya hoja zisizo na mashiko.Kama hujui kwanini tunazaliana sio vibaya ukapitia upya tena hata maandiko ya Mungu ili uone hata huko lengo kuu halisemi  kuzaa ili watoto waje kukulipa fadhila kwa malezi yako na kama hapo bado haitoshi basi Jaribu kukaa na wazee hasa wenye umri wa miaka sitini utasikia wengi wao wakilalamika kuwa watoto wao hawawasaidii ila usikomee hapo nenda kafuatilie maisha ya hao wanaopewa lawama utakuta maisha yao bado pia yanahitaji utegemezi yaani bado hata wao hawajajimudu sasa swali ni je ni sawa kulaumiwa?

Kama sio changamoto mfano kubakwa na kusababishiwa ujauzito basi usikurupuke kuwa mzazi ilihali hujajua kwanini unatakiwa kufanya hivyo.


Usiwe  mzazi kwa ulimbukeni tu  bali jiulize upo tayari kulipa gharama za kuwa mzazi? Au ndio unataka uwe yule mzazi ambaye anatoa malezi kwa mkopo ili baadaye alipwe?

Kuna watoto hawasemi tu ila ukweli wanashindwa kuwaelewa wazazi wao kwa sababu mpaka wanatamkiwa maneno ya laana kwa sababu tu hawataki kuwalipa fadhila wazazi wao , wazazi wamekuwa wakiwatamkia maneno makali na kusema bila aibu kuwa waliuza sijui nyumba ili watoto wasome sasa huo ni wajibu wa mzazi kumuandaa mtoto ikiwemo kumpa elimu sio uje kumdai baadaye naye akulipe.

Mzazi jiandaye vizuri kabla ya kuwa Baba au mama na elewa kuwa utatakiwa kuwajibika kimalezi bila kufikiria kulipwa fadhila.

Watoto wengi wamekuwa wanaishi kwa kukosa utulivu kwa sababu wanalazimishwa kuwajengea wazazi nyumba bila hivyo wanatishiwa kupewa laana sasa Kama umri wako wote wa ujana umeshindwa kujenga na tena usikute ni kwa uzembe wako tu iweje uwabane watoto wakufanyie hivyo na kibaya zaidi unakuta ndio kwanza mtoto kapata ajira au ndio kwanza anajitafuta ila tayari mezani umemlundikia matatizo yote ambayo wewe ukiwa na nguvu yalikushinda.

Kushindwa kujiandaa kwako mzazi ni chanzo cha matatizo kwenye familia za watoto wako kwa sababu mtoto ataogopa mpaka kuoa kwa sababu tu akijiongezea majukumu atashindwa kukuhudumia wewe na kwa wale ambao watalazimisha kufanya hivyo basi itazuka vita kati ya mzazi na mkwe wake kwa sababu mzazi ataamini hajaliwi kwa sababu mkwe ameingilia kati.Kwa mtoto wa kike naye ndio pale analazimishwa kuolewa na mtu mwenye pesa tu ili awe Kama kitega uchumi na kama sio hivyo basi ndio akiolewa anabanwa awe anatuma pesa mara nyingi mwisho wa siku mumewe anagundua hivyo tayari ndoa inaanza migogoro na yote hayo ni kosa tu la mzazi Kushindwa kujiandaa kujitegemea na kutaka watoto wamlipe fadhila.


Mzazi tambua kuwa kumtunza mtoto ni wajibu wako sio kumkopesha na jukumu la kujitunza wewe ni lako japo watoto wanaweza kukusaidia ila sio kitu cha kutegemea kwa sababu na wao wana majukumu ya kuanzisha familia na kujitafuta pia kiuchumi ili uzao uendelee, ukizeeka au ukawa unaumwa na huwezi kujimudu basi hapo watoto watachukua jukumu la kukutunza ila bado una nguvu na sio mzee unaanza kuwabana watoto wakulipe fadhila je wakaibe ? 

Kushindwa kujiandaa kwa mzazi ndio mwanzo wa kulaumiana kwenye familia mpaka ukoo na hii ni pale ambapo watoto wako mwenyewe unataka ndugu wakusomeshee na wakisema hawawezi tayari unawatupia lawama nyingi  tena bila aibu unaongea hata mbele za watu kuwa kina fulani hawataki kusomesha watoto zako ilihali wana pesa bila kufikiria kuwa na wao wana mizigo yao pia hata kama wana pesa ila unajua bajeti zao? Kilichofanya yote hayo ni wewe hapo kwanini lawama wapewe wengine?

Mzazi kamili hujiandaa yeye na kuwaandalia watoto pia na kwa kufanya hivi ni rahisi kuvunja mnyororo wa umaskini kwa watoto wakizaliwa wanajipambania  wao na wajukuu zao na sio tena uwape familia nyingine yaani wapambane kwa ajili ya watoto wao na huku pia wakupambanie wewe. 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha 

+255652 134707

No comments:

Post a Comment