Sunday, 13 March 2022

MBINU ZA KUWEKA AKIBA

 JINSI YA KUWEKA AKIBA 

Elimu ya pesa kila siku inakuwa changamoto mpya kwa watu wengi ndio maana  bado kuna watu wanaingiza pesa ya kutosha lakini matumizi yao sio rafiki kiasi cha kuwafanya wabaki na ziada ya pesa . Inawezekana hata wewe ukawa kwenye kundi hilo la watu ambao wanaweka malengo ya kujikomboa kiuchumi kila siku lakini utekekelezaji wake ni mdogo au haupo kabisa, ukijiona wa hali hiyo basi tambua una changamoto katika namna nzima ya kuitawala pesa  na njia rahisi kwa watu  hali zote za vipato ni uwekaji wa akiba na mipango madhubuti ya namna ya kuizalisha hiyo akiba ili nayo ilete faida. 

Akiba kwa tafasiri isiyo rasmi ni namna mtu anavyoijali kesho yake ndio maana leo unajinyima ili kesho ufanikiwe katika jambo fulani , mfano  unaingiza shilingi elfu kumi kila mwezi na unataka baada ya mwaka uwe na mtaji wa laki mbili hapo lengo ni wewe upate mtaji wa laki mbili lakini mfukoni una shilingi elfu kumi ambayo kila mwezi utaipata, kwa kawaida unaweza kuiona ndogo lakini  kuna uwekano mkubwa mtu asiifikishe kwa mwaka .

Kuna elimu nyingi kuhusu uwekaji wa akiba ambazo hutolewa kila leo na pengine ukawa moja kati ya watu ambao tayari wamewahi kuzitumia njia hizo lakini bila mafanikio yoyote, unafikiri tatizo ni nini?  Kuna kitu muhimu kutambua kabla ya kuanza zoezi la kuweka akiba ya pesa nacho ni wazo kuu la kesho, jiulize kesho unataka ufanye nini?  na ili ufanikiwe jambo hilo wahitaji kiasi gani cha fedha?  Ukifahamu kiasi cha fedha unachohitaji ili kufikia lengo hilo utatakiwa kujua kwa sasa wewe unapata kiasi gani cha fedha? iwe ni kwa mwezi au kwa kila siku muhimu uwe na uhakika na kiasi hicho cha fedha. 

Ukijua unaingia shilingi ngapi labda kwa mwezi sasa utatakiwa ujue pia matumizi yako kwa mwezi yakoje? Yanagharimu kiasi kipi cha fedha?  Na je matumizi yako kwa siku mpaka mwezi yanakuruhusu uweze kuyafikia malengo yako? Ukiwa na majibu ya maswali hayo ndipo utaangalia sasa kipi kinawezekana kupuguzwa ili matumizi yako kwa mwezi yapungue. 

Hatua ya pili ni kuorodhesha matumizi yako katika safu mbili , moja iwe ya matumizi ya lazima mfano chakula  n.k na ya pili iwe ni ya matumizi yasiyo ya lazima kisha  tafuta uwezekano wa kupunguza matumizi yasiyo ya lazima ili pesa ambayo ilikuwa inatumika kwenye matumizi hayo  iingie kwenye akiba na pia uanze kujinyima kimatumizi  ili upate pesa ya ziada .

Hatua ya tatu ni kujiwekea mikakati ya kujikumbusha malengo yako kwa mfano unaweza kuwa na utaratibu wa kila siku jioni unapitia daftari lako la malengo ili uwe na shauku ya kuendelea na mapambano bila kuchoka. Unatakiwa Kuheshimu mikakati yako kwa kuwa na nidhamu katika  kuweka akiba ili uweze kufikia malengo yako. 

Hatua ya mwisho ni kuhakikisha pale upatapo pesa  unatoa kwanza kiasi ambacho umeridhia kukiweka kabla ya matumizi mengine yoyote  usifanye makosa kwa kuanza kutumia pesa kwanza kisha ndio ubakize akiba , fanya zoezi hilo kwa nidhamu yote na lifanye kwa kuongozwa  na malengo ya kesho.

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

+255652 134707 

Friday, 18 February 2022

MBINU ZA KUISHI NA WATU WENYE TABIA NGUMU

MBINU ZA KUISHI NA WATU WENYE TABIA NGUMU MAKAZINI. 

Kama sio wewe basi utakuwa umewahi kutana na mtu akilalamika dhidi ya watu ambao wana tabia zisizo rafiki na pengine mpaka mtu huyo anatamani kuachana na kazi hiyo ili aepuke kukutana na watu hao , ni kweli wapo watu wana tabia ambazo ni ngumu kuvumilikika kiasi kiasi cha kufanya wengine wakose amani pindi wakiwa na watu watu hao wenye tabia zisizo rafiki. 

Pengine hata wewe kuna mtu ana tabia ambazo zimekufanya ujiulize swali hili " hivi huyu mtu anaishije na familia yake kwa tabia hizi?" Maana kama yuko hivyo kazini inakuwaje nyumbani kwa ndugu zake ambao wengine analala nao kitanda kimoja  na kula nao meza moja si pengine ikawa kila siku makwazo kwenye nyumba hiyo ? Lakini ukweli ni kuwa hakuna makwazo kabisa anaishi na familia yake vizuri tu kwa sababu  walipomfahamu walijifunza kuishi naye kwa kumzoea alivyo  changamoto ipo kwako ambaye hujazaliwa naye bado hujajifunza kuishi naye na pengine hutaki kujifunza kuishi naye. 

Hakuna namna utaishi bila kukutana na watu wenye tabia zote nzuri na mbaya ili uepuke hilo basi kajifungie kisiwani peke yako lakini tofauti na hivyo lazima utakutana na watu wenye tabia zote nzuri na mbaya sasa itategemea na watu hao umekutana nao wapi na wana nafasi gani kwako  kama ni kazini na ofisi moja je utaacha kazi kwa sababu ya watu hao?  Au utakuwa unakaa nje ya ofisi kuwakwepa watu hao ? Haiwezekani hilo na sio suluhisho lake lazima ujifunze kuishi nao watu hao. 

Jitahidi ujue mnapishana sana kwenye kipi kwa sababu sio kweli kwamba mtapishana kwenye kila kitu lazima tu kuna sehemu moja  ndio huwa chanzo cha kupishana naye na ukilitambua  eneo hilo basi tenga siku moja tafuta eneo tulivu jitafakari ni kwa nini mtapishana? na kwa nini eneo hilo? Anza kutengeneza mbinu za kuishi naye mtu huyo kwenye eneo hilo na moja wapo ya mbinu nzuri ni kutojibana naye sana kwenye eneo hilo jifunze kupuuzia baadhi ya kauli zake , pengine uone ugumu kukaa kimya pindi anapoongea kama tabia yake ilivyo lakini baadaye utazoea tu na itakuwa akiongea mambo yake unajibu machache mengine unamsikiliza. 

Mbinu nyingine ni kumpuuza kwenye baadhi ya mambo yake lakini usimuonyeshe kuwa unampuuza bali usifanyie kazi kila tukio lake kwako kwa mfano mmekutana kazini umemsalimia hajaitika au yeye hakusalimii  hilo lisikupe msongo wa mawazo kwa kujiuliza kwa nini haitikii salamu zako bali mpuuzie tu kwa sababu ndivyo alivyo na usiache kutabasamu pindi ukikutana naye na wala usilipe kisasi kwa anayokufanyia  na hapo itakuwa mwanzo wa wewe kuishi naye mtu huyo. 

Mbinu nyingine ya tatu ni kujitahidi unaepuka mazingira ya kukaa na mtu huyo muda mrefu ila isipokuwa pale tu inapobidi kwa sababu za kikazi tofauti na hivyo muepuke mtu huyo kwa kujishugulisha na mambo yako mengine. 

Mbinu nyingine ni usiitizame tabia yake kama kikwazo kwako bali muone kama ndivyo aliumbwa hivyo na ukiliweza hili basi usiwe unamuongelea jinsi alivyo mbele ya wengine bali muombee kubadilika kwa sababu tabia yake sio kwamba unaiyona wewe tu bali kuna wengine pia wanaiyona hivyo tabia yake inakuwa kikwazo kwake sio kikwazo kwako wewe kazi yako ni moja tu kujifunza kuishi naye 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha


+255652134707

Tuesday, 1 February 2022

ELIMU YA PESA

 USISUBIRI PESA IPUNGUE NDIO UWEKE NIDHAMU YA MATUMIZI

Matumizi ya pesa bado ni changamoto kwa watu wengi na matokeo yake ni hujikuta katika ukosefu wa pesa mara kwa mara na hii sio kwa waajiwa tu hata waliojiajiri kwenye mambo binafsi  bado hujikuta kwenye kipindi kigumu cha ukosefu wa pesa sio kwa sababu haikuwepo la hasha ni kwa sababu ilikuwepo lakini ikatumiwa bila kuzingatia matumizi sahihi kutokana na kipato. Ukipata muda tulivu ukajitafakari utagundua kuwa pindi upatapo pesa matumizi yako yanakuwa juu na hupungua kadri pesa inavyopungua yaani kwa lugha rahisi  ni kuwa nidhamu yako ya matumizi ya pesa inaongezeka kadri unavyoishiwa pesa. 

Pesa ni nguvu ya kihisia ambapo usipoitawala itakutawala yenyewe kwa kukupa maamuzi mengi na hapo utakosa utulivu hali ambayo itafanya upoteze nidhamu ya matumizi ndio maana mshahara ukiingia unaweza jikuta unafanya manunuzi bila kuangalia ukubwa wa gharama kwa sababu unajua pesa ipo lakini ukianza kusikia mfuko umepwaya ndio utarudisha makini wa matumizi kwa mfano mwanzo ulilipwa laki tano na ilipofikia mfukoni umebaki na laki moja ndio utaanza kuipogia mahesabu hiyo laki moja kuangalia kama itakufikisha mwezi mwingine, je kwa nini hukufikiria hivyo tangu ukiwa na laki tano? 

Nidhamu ya pesa ni kuheshimu pato lako kwanza na pili ni kuheshimu matumizi sahihi yaliyo ndani ya kipato chako kama ulipanga kununua kitu cha shilingi mia ndio itakuwa sawa kulingana na kipato chako basi fanya hivyo lakini ulinunua kwa shilingi Mia mbili ujue umekula na pesa ya siku fulani hivyo jiandaye siku hiyo kukosa pesa la sivyo iwe ni dharura ndio tumia lakini kama si dharura yatakiwa ujidhibiti dhidi ya matumizi ya pesa pale tu unapoipata, changamoto ya pesa ni kuwa ukitumia pesa ndogo unaona kawaida tu lakini mwisho wa siku ukijumlisha unakuta kama ungehifadhi ungekuwa mbali sana kifedha hivyo nidhamu ukianza na kuheshimu matumizi yako yaliyo ndani ya kipato chako utakuwa kwenye kiwango kizuri cha kuweka akiba. 

Nidhamu binafsi katika matumizi ya pesa inajengwa na lengo kuu ulilonalo la kesho hapo ndio utakuwa unatumia pesa ukikumbuka kesho hivyo utakuwa ukijikumbusha kila kabla ya matumizi ambayo si salama kulingana na kipato chako na utakuwa na nidhamu muda wote, lazima uwe na nidhamu au ukose nidhamu lakini ukubali kupoteza lengo kuu la kesho na njia nzuri nyingine ni kuigawa pesa yako kwa siku utagundua unaingiza shilingi ngapi kila siku na kisha angalia matumizi yako kila siku yanaendana na pato lako la siku? Kwa kuanzia na hapo utajirekebisha kimatumizi na utaheshimu matumizi sahihi ya pesa. 

Pesa ikiwa nyingi itakupa upofu uuamini kuwa huwezi kuishiwa hivyo kila matumizi yakujiayo kichwani utayafanya na hapo ndio mwanzo wa kutumia hovyo pesa  mpaka baadaye ikipungua ndio itakutoa upofu uone kuwa kuna hatari itokanayo na ukosefu wa pesa kwa sababu pesa uliyonayo haitoshi kukufikisha msimu mwingine wa pesa kumbe kuna kuna nguvu kubwa inatakiwa uwe nayo awali ili kudhibiti hisia za pesa zisikutawale. 

Kujua unataka nini pia ni moja wapo wa ujenzi mzuri wa nidhamu ya pesa kwa sababu utajizuia dhidi ya matumizi ambayo sio ya msingi kwako na hayapo ndani ya bajeti yako kwa kipato chako na aina yako ya safari uliyonayo, kutojua nini unataka itakuingiza kwenye matumizi yasiyo sahihi kwa sababu kila utakachokiona kinavutia utahitaji kukinunua. 


Mwanasayansi Saul Kalivubha 

0652 134707

Thursday, 7 October 2021

USIJISAHAU KWENYE MAZINGIRA HAYA

 USIJISAHAU KWENYE  MAZINGIRA HAYA. 

Habari ndugu msomaji wa makala zetu za fikia ndoto zako ikiwa ni muda kidogo umepita bila kukuandikia makala kupitia blogu leo tena ni siku ya bahati ya pekee kukuandikia makala hii maalum, ni makala maalum kutokana na ujumbe wake kuwa mchungu kuumeza lakini muhimu na wenye manufaa ikiwa utakubali kuumeza, karibu sana tuambatane. 

Kama ilivyo kichwa tajwa hapo juu somo linahusu kutojisahau katika mazingira upitiayo na kabla sijaendelea  sote kwa pamoja tujibu maswali haya kimya kimya;

#Umewahi kujutia kwa kutamani siku zirudi nyuma utumie mazingira fulani kufanya jambo zuri la maisha yako? 

# Umewahi kuwa na nafasi ambayo ilikuruhusu ufanye jambo fulani na sasa huwezi tena kulifanya kutokana na wewe kuwa nje ya nafasi hiyo kwa sasa? 

#Umewahi kuona watu wakiwa maarufu na sasa tena unawaona wakiwa katika hali ambayo hakuna anayetamani kufahamu habari zao ?

Bila shaka kuna majibu yanakujia akilini kuwa kuna nyakati na jambo ndani ya nyakati hizo ambalo ukilifanya hutojutia ( hapa nazungumzia jambo lenye matokeo chanya), ugumu ni utatambuaje nyakati hizo zimebeba jambo lipi? 

Kila nyakati kuna kusudi la wewe kupitia humo hilo ndio jambo kuu ambalo unatakiwa kulifanya kwa juhudi zote ikiwezekana kwa kipaumbile kikubwa zaidi kwa mfano ukienda shule kuna mambo mengi ya kufanya lakini kuu ni kusoma kwa bidii ili baadaye usitamani tena kurudia shule ili usome kwa bidii wakati huo utakuwa haiwezekani tena pengine. 

Unapopitia mazingira fulani penda sana kutafuta lengo kuu la wewe kuwa hapo na jitahidi kulifanya kwa juhudi zote, karibu kila mtu ana wakati wake wa kuwa bora katika eneo fulani hapo ndipo hupaswi kulewa mazingira bali kusimama kweli kwenye nafasi yako kwa sababu ubora huo unakuandaa kuwa mtu fulani kesho.

Maisha ni makusanyo wa nyakati mbali mbali unazopitia leo mpaka kufikia kesho utakuwa mtu mwingine tofauti kutokana na alama ulizojikusanyia kwenye nyakati hizo ulizopitia  hivyo sio wakati wa kubeza na kujisahau kwa nyakati unazopitia tafuta ubora wako uko wapi na uishi ubora huo kwa juhudi zako zote. 

Makala hii imeandikwa na  Saul Kalivubha 

Mwanasayansi tiba 

+255652134707

Wednesday, 28 July 2021

WAFAHAMU WATU HAWA WAWILI HATARI KWENYE MAISHA YAKO

 WAFAHAMU WATU HAWA WAWILI HATARI KWENYE MAISHA YAKO. 

Urafiki ni hisia zisizo epukika ndio maana sio rahisi kuishi peke yako hata uwe na tabia gani mbaya lazima umpate rafiki ambaye mtakuwa nnaweza kupikika chungu kimoja na hiyo ndio maana halisi ya urafiki ni hisia, lakini kwenye eneo hilohilo ndipo kuna vilio vingi sana vya watu kuumizwa , je nawe umewahi kuumizwa? 

Katika maisha ya urafiki kuna makundi makubwa matatu ya watu ambao watakuja kwako ambayo ni WAPITAJI, WAKAAJI na WAFANYA MAJARIBIO sasa ukiweza kufahamu elimu hii vizuri kuna uwezekano mkubwa ukawa hupati shida sana kwenye kutibu majeraha yako yatokanayo  na maumivu ya urafiki. 

 WAPITAJI: Hili ni kundi ambalo ni kubwa sana yaani namaanisha utakutana na wapitaji wengi sana kwenye maisha yako na kuitwa wapitaji haimaanishi kuwa sio watu wazuri kwenye maisha yote la hasha ni watu wazuri tena sana lakini kosa lipo kwako unapolazmisha wapitaji wawe marafiki wa kudumu kwako. 

Wapitaji ni watu wazuri ikiwa utakubaliana na kanuni ya asili kuwa muda wake ukifika wa kuondoka utamwacha aondoke na kwa nini aondoke? Ni kwa sababu kusudi lililomleta kwako limeisha kwa mfano ikiwa kuna mtu alikuja kwako ili tu mshirikiane kimasomo basi mkimaliza shule kuna uwezekano mkubwa urafiki ukapungua na kabla hujambadilishia nafasi nyingine kaa chini jitafakari uone ni kweli atakuwa bora tena hata kwenye nafasi nyingine utakayompa? La sivyo muache aende tu usilazimishe abaki. 

WAFANYA MAJARIBIO; Hawa ni watu ambao wapo kwenye makuzi ya kujifunza na mara nyingi hutokea sana kwenye urafiki wa kimapenzi ndio kuna watu watakuja kwako kwa minajiri ya mahusiano lakini sio kwa sababu wana lengo kuu na wewe la kesho ( future) bali ni kwa sababu ndio kwanza mahusiano kwao imekuwa starehe ya kwanza hivyo wanataka tu mcheze michezo ya kimahusiano, watu hawa mara nyingi utawagundua kwenye namna wanavyosuasua kwenye kuwa na subira na kuipanga kesho yake ikiwa pamoja nawe kwa lugha rahisi ni watu ambao wanahitaji mahusiano ya kutimiza hisia za mwili tu na sio mengineyo.

Makala hiii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

0652134707

Saturday, 19 June 2021

ELIMU YA DARASANI HAITOSHI JIFUNZE NA HIZI

 WANAFUNZI TUJIONGEZE ZAIDI YA ELIMU YA DARASANI 

Tupo katika zama ambazo ajira ni changamoto kubwa sana sio katika nchi yetu tu bali Duniani kote kilio ni kimoja kwa wasomi wengi  lakini tukiachana na tatizo la ajira bado kuna maisha mengine nje ya shule yamekuwa changamoto sana kiasi cha wahitimu kupachukia uraiani  kwa mfano maisha ya mahusiano, maisha ya kujitegemea, elimu ya pesa n.k

Jamii mara zote humuandaa mtoto aende shule kwa lengo kuu aje kuwa na maisha bora baadaye na hata mwanafunzi mwenyewe kadri anavyozidi kuvuka viunzi vya kielimu kuelekea elimu ya juu ndivyo anakuwa na imani kuwa shule itampa maisha mazuri lakini baadaye anapohitimu  hukutana na maisha tofauti kabisa mtaani hata kama atapata ajira lakini utakuta elimu ya pesa inamsumbua au alimu ya namna ya kuishi na watu inamsumbua.

Kitu ambacho ni kigeni kwa wanafunzi wengi huwa wanasahau kuwa shuleni tunaenda kusomea taaluma kwa sehemu kubwa mfano Dakitari wa binadamu miaka mitano yote huandaliwa kumtibu binadamu, Mwanasheria miaka yake minnne huandaliwa kuja kuitafasiri sheria kwa vitendo, mwalimu miaka yake mitatu huandaliwa kuja kumfundisha mwanafunzi mbinu mbali mbali za kufaulu mitihani na kujua kuandika na kuhesabu n.k , ukitazama mifano hiyo utagundua kuwa  shuleni tunaenda kujifunza namna ya kuitumikia taaluma katika mazingira husika na sio namna ya kukabiliana na mazingira ili maisha yawe mazuri. 

Maisha ni zaidi ya taaluma kwa sababu ukihitimu maisha yako yatakuwa sio kutibu tu au kufundisha tu bado utahitaji uwe na familia, utalipwa mshahara na utatakiwa uutumie vizuri, utatakiwa ujitegemee kimaamuzi sasa swali ni je elimu hizo utafundishwa darasani? ndio maana kuna umuhimu mkubwa wa kujifunza zaidi mambo nje ya taaluma yako na njia pekee na rahisi kujifunza mambo nje ya taaluma ni kusoma vitabu vya stadi za maisha vilivyoandikwa na wabobezi katika maeneo mbalimbali ya maisha, kuna maeneo muhimu ya kujifunza ambapo unaweza kuwa unafanya kwenye muda wako wa ziada  ukawa unajisomea vitabu

Elimu ya pesa ni elimu ambayo ni muhimu sana kwa sababu matokeo ya kuitumikia taaluma yako ni kulipwa pesa lakini una elimu ya kuitumia pesa yako? tafuta vitabu vya pesa vilivyoandikwa na wabobezi katika eneo hilo jifunze mbinu mbali mbali za namna ya kuzalisha pesa kwa kutumia mshahara wako au mkopo wako, vitabu vitakupa mbinu za kuweka akiba na kutumia pesa uliyonayo kutafutia pesa usiyokuwa nayo. 

Elimu ya  mahusiano pia ni elimu ambayo ni muhimu sana katika maisha kwa sababu utahitaji uwe na familia na wewe utakuwa baba au mama katika familia sasa utawaongazaje wana familia?  vitabu vimeeleza mengi na wabobezi hivyo vitakufunza Ujasiri katika kuyakabili mazingira ya kimahusiano, mbali na mahusiano ya kimapenzi bado kuna mahusiano ya wafanyakazi hivyo utatakiwa uwasiliane nao vyema la sivyo utachukiwa kazini kila siku na watu kwa tahitaji zako

Elimu ya kujitegemea hii ni elimu muhimu sana kwani uwezo wako utapimwa kwenye namna unavyoweza kujitegemea kwa kufanya mambo hata siku utakayokuwa peke yako, elimu hii pia ipo vitabu muhimu tu uchukue vitabu ambavyo vimeandikwa na wabobezi katika eneo hilo.

Elimu ya biashara pia ni elimu muhimu sana kwa sababu maisha ni biashara unaweza usiifanye moja kwa moja lakini usisahau kuwa hata ukienda sokoni kufanya manunuzi tayari hiyo ni biashara au ile namna ya kuitumia mshahara wako ili ukifikishe mwezi ujao hiyo ni biashara tayari kwani utatakiwa utoe vipaumbele vya kimanunuzi ili ubaki na salio , elimu hii ipo vitabu imeandikwa na wabobezi katika eneo hilo la  biashara hivyo kazi ni kwako tu kujipangia ratiba rafiki.

Elimu zaidi ya taaluma kitakufanya uwe na mbinu nyingi za kuyakabili maisha mbali na kuitumikia taaluma yako bado utaweza kuzikabili changamoto mbalimbali za maisha 


Saul Kalivubha ni Mwanasayansi tiba na mwandishi 

0652 134707

Monday, 22 February 2021

MIAKA 29 YA SAUL KALIVUBHA

 Karibu katika blogu yetu ya fikiandotozako na kama ilivyo ada leo nitajibu maswali ambayo yaliuzwa katika siku yangu ya kumbukizi ya kuzaliwa tarehe 22 February , maswali yalikuwa jumla 150 na nilipitia yote ijapo yalikuwa sehemu mbili tu 

Mahusiano 

Mafanikio binafsi 

Mahusiano, hapa maswali yalikuwa mengi sana zaidi ya robo tatu yalikuwa ni maswali ya mahusiano sikushangaa sana kuulizwa maswali mengi namna hiyo kwa sababu mfumo wangu wa maisha moja ya eneo ambalo silionyeshi wazi ni mahusiano na mafanikio yangu binafsi.

Kwa sasa watu wengi hupima mahusiano ya mtu mitandaoni na ukifuatilia kurasa zangu sijawahi chapisha ( post) chapisho lolote iwe picha au maneno yenye viashiria vya mahusiano huo ni utaratibu wa mtu mwenyewe kwangu upo hivyo sina maana kuwa anayeweka wazi mitandaoni anakosea la hasha.Wengi waliuliza nitaowa lini na nitamuoa nani? 

Katika mahojiano fulani niliwahi kuzungumza kuwa siku nikitoa kitabu changu cha tatu itakuwa sambamba na harusi yangu na tayari michakato ya kutoa kitabu hicho cha jina la NTAOWA BILA UCHUMBA ipo mbioni kwa hiyo sina haja ya kusema siku bali tusubirie, nani nitamuoa?  nikijibu swali hilo itakuwa nimerudi kule kule kupost ( chapisha mirandaoni) hivyo mniwie radhi kwa hilo siku ikifika kwa mwenye kutaka kumjua atamjua. 

Sipendi sana kuweka maisha binafsi mitandaoni kwa sababu kuu mbili;

1.Maisha binafsi sio biashara niitangaze 

2.Huduma zangu mitandaoni sio kuwaambia watu ninaishije bali kuwaonyesha matokeo ya ninavyoishi ikiwemo kuhamasisha kwa kilicho ndani ya uwezo wangu 

Mafanikio binafsi,watu walitaka kujua uandishi umenipa nini mpaka sasa ni kweli nina miaka minne sasa kwenye tasnia hii na kwanza kabisa kama mafanikio kwangu ni kujiweka kwenye orodha ya watu kama msaidizi wa mafanikio yao hayo ndio mafanikio zaidi kwangu lakini pia mafanikio ya kiuchumi kwa uandishi yapo pia kwa sababu kuna kipindi nimeishi karibia mwaka sina kazi yoyote tofauti na uandishi na maisha yaliendelea,pia kupitia uandishi niliweza kununua mshamba nikalima na kiasi fulani nikaingiza kwenye ujenzi wa nyumba yangu.Nimedokeza machache na kuvunja utaratibu wangu wa kutoweka wazi maisha binafsi bali nimefanya hivyo kama hamasa kwa watu kuwa hatuapaswi kuchoka na safari 

Maisha ya uandishi ni kipaji hivyo tokea nitambue hilo nikaamua kuayapa nafasi kwangu kwa sababu kuna watu wanauliza naweza vipi ilihali nimesoma afya? Inawezekana kabisa ni suala la nidhamu tu nikiwa kwenye mambo ya afya nakuwa makini huko nikitoka mashmabulizi huamia kwenye uandishi. Uandishi nina ufanya kama sehemu ya maisha lakini miaka ya mbele itakuwa ndio shughuli yangu kuu.

Mashairi ni kipaji? Mashairi ni kipaji ijapo pia mtu anaweza kusomea hivyo kwangu ni kipaji lakini baadaye nikajiboresha huko zaidi kupitia vitabu

Kwanini riwaya ya NTAOWA BILA UCHUMBA?  hiyo ni hadithi tu ambayo nimeamua kuiandika na sina maana kuwa nitaowa bila uchumba na pengine zama zetu hizi ikawa ngumu kufanya hivyo kwa sababu inahitaji muda kukaa na mlengwa ili mufahamiane katika mbili tatu kisha ndio hatua nyingine ifuate lakini kwenye hadithi hiyo nilimaanisha  hakuna haja ya uchumba bandia .

Kila mtu anatamani kufikia eneo fulani kimafanikio na hiyo ndio chachu inayochochea upambanaji wa mtu husika kama hauko tayari kuyasaliti malengo yako lazima kila siku ujitume 


Mwanasayansi Saul Kalivubha 

0652 134707