Sunday, 12 November 2023

EPUKA MARAFIKI HAWA ILI UFANIKIWE

 KAMA UNA MARAFIKI HAWA HUWEZI KUFANIKIWA  


Marafiki ni sehemu ya maisha ya kila siku maana sio rahisi kuishi bila marafiki hata mtu awe na tabia ngumu vipi kiasi cha kuonekana havumiliki ila tambua ana marafiki ambao wanamvumilia na tena wanapendana. Kitu ambacho wengi hatukijui ni mahusiano kati ya marafiki na mafanikio, kuna mahusiano makubwa kati ya mafanikio yako na aina ya marafiki ulionao ndio maana kuna mwandishi na mwanafalsafa maarufu aliwahi kusema mafanikio yako ni wastani ya marafiki zako watano ambao mnatumia muda mrefu kuwa pamoja, kwa ufafanuzi wa haraka ni kuwa ukimuona maskini mmoja jua kuna maskini wengine watano anaoshirikiana nao na ukimuona  tajiri mmoja jua kuna matajiri watano anaoshirikiana nao .

Marafiki ni chachu ya mafanikio yako kwa sababu  ni ngumu kuwa na rafiki mfanya biashara ilihali wewe huna biashara kwani maingezi yenu yatapishana tu na kama ikitokea hivyo basi jua kuna unafiki kati yenu yaani maongezi yenu hayana maana na hakuna urafiki hapo kwa sababu.

Kabla hatujaenda kwenye marafiki wa kuwaepuka hebu angalia mifano hii na kisha jichunguze uone ukweli ulivyo.

Mtu ambaye anafeli sana jambo fulani Jaribu kuchunguza marafiki zake utakuta wanafarijiana kuhusu kufeli kwao.

Mtu ambaye ana starehe nyingi ambazo zimeguka kuwa kikwazo chake cha mafanikio Jaribu kumfuatilia utakuta ana marafiki ambao anashirikiana nao na wanajiona wapo sahihi kabisa kufanya hivyo ndio maana wanaendelea.

Ukiona mtoto kuna tabia haachi jua kuna mtu anamuhamisisha kuendelea nayo hiyo tabia. 

Umeona mifano hiyo ? Bila shaka umepata mahusiano kidogo na pengine hata wewe kuna jambo unaendelea nalo kwa sababu kuna mtu nyuma ya jambo hilo , na mfano wa mwisho ni huu hebu angalia michango ya mtu maskini akiwa ana jambo lake kama harusi na kisha angalia michango ya jamaa zake kisha fanya hivyo hivyo kwa tajiri hapo utagundua kila mtu kachangiwa na marafiki wanaofanana uwezo  na hapo ndipo tunarudi kwenye ule ukweli kuwa upo sawa na marafiki zako.

Kuna marafiki ambao unatakiwa kuwakwepa  na kama unao basi tambua kuna hatua hutaziona za kimafanikio, marafiki hao ni hawa wafuatao :

Wanaolalamika sana;hawa watakuambukiza tabia ya kukwepa kuwajibika kwa makosa yako mwenyewe kwa sababu kwa tafasiri ya haraka ya mtu mlalamikaji ni kuwa haoni kuwa anakosea bali muda wote anaona wengine ndio wenye makosa na mwisho wa siku mtu anayelalamika sana huwa anaishia kuwa mtumwa wa wengine, ukiwa na marafiki hawa sio muda mrefu nawe utaanza kuwa mlalamikaji na kunyonyeshea vidole wengine kila muda. 

Marafiki wenye mitizamo ya kimaskini, hawa ni wale ambao wameridhika na hali zao za kuteseka na ukosefu wa fedha yaani tayari wameukubali umaskini, watu hawa wanakuwa na kauli nyingi za kutetea umaskini wao na pia huwa ni wavivu wa uthubutu  kwa sababu tayari wameshahalalisha umaskini wao na utawasikia mara nyingi wakijificha pia kwenye imani za Mungu kama vile kusema ni mpango wa Mungu wao kuwa hivyo na wengine huanini utajiri ni dhambi hivyo kila tajiri wanamuita mshirikina( freemason) ,Kaa mbali na watu hao watakuambukiza umaskini na ikitokea ni ndugu zako ambao huwezi kuwakwepa basi jua una kazi kubwa ya kufanya kutengeneza ukoo tajiri kutokea kwako.

Marafiki wanakutafuta tu kwenye uhitaji, hawa ni wale watu ambao kila mkikutana lazima kuna jambo upoteze , yaani ukiona simu yake tu basi jua lazima mazungumzo yenu yaishie na wewe kumpa kitu au kutoa ahadi utampa lini na ni  siku chache sana wao kukutafuta kwa mijadala mingine ya kimaisha, hawa watu hawakupa mawazo mapya bali wanakufanya uwafikirie wao tu tena kwa kuwapa vitu.Kusaidiana ni sehemu ya maisha ila epuka watu ambao muda wote wamekugeuza kituo cha msaada kwa sababu usipokuwa makini watakugruza mtumwa wao yaani watajiona muda wote wana haki ya kusaidiwa na wewe na siku ukikosa watajua umefanya makusudi watasahau siku ulizowasaidia na kuanza kukulaumu na kumuona yule ambaye hajawsaidia hata siku moja ndio mtu mzuri anayefaa.

Marafiki wanaotaka wewe tu ndio uwatafute, Kaa nao mbali kabisa tena ukiweza futa hata mawasiliano yao na kama ni ndugu  basi ishi nao kama wanavyoishi na wewe acha kuwatafuta mpaka pale kwenye ulazima wa kufanya hivyo kwa sababu ukikubali tu kuwa mtu wa kuwatafuta wewe muda wote jua utakuwa mtumwa wao na utaanza kuwafikiria wao muda wote hali ambayo itafanya ushindwe kufikiria ya kwako vizuri na ushindwe kwenda mbele kwa sababu wao wapo nyuma maana huo ujasiri utaukosa na usipokuwa makini utajikuta kwenye madeni ya kukopa mpaka muda wa maongezi ili tu uwasiliane nao na huku kwenye simu zao wana salio la kutosha , mtu ambaye anataka wewe tu ndio umtafute sio kwamba hiyo ni tabia yake bali kisha ona udhaifu wako na hili uthibitishe hilo fuatllia watu wake wa karibu je anawafanyia kama wewe?

Marafiki wajuaji , hawa ni wale ambao wanakukosoa hata kabla hawajakusikiliza na tena wanamalizia ulichokianzisha bila kujua ungemaliziaje, hawa ni marafiki hatari sana usiruhusu muda mwingi kuwa nao kwa sababu watakufunza ubishi usio na faida.

Marafiki waongo na wambea, Muongo ni mtu ambaye anakusambizia au kukuzuishia habari za uongo ila mmbea yeye ni yule ambaye anakusambazia habari za kweli ila bila idhini yako na kwa watu ambao hawakutakiwa kuzijua hizo habari, hao ni watu hatari sana kwa sababu watakufanya mweupe kwa kutoa siri zako na kufanya rahisi kwa adui zako kukushambulia na ukiwa na marafiki hao yawezekana mipango yako ikawa inasindwa kila mara kwa sababu kuna muda inanidi watu waone tu matokeo na sio maandalizi kwa sababu watakuzuia .


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul kalivubha, mtafiti 


+255652 134707

Saturday, 20 May 2023

HIZI NDIO SABABU ZA KWA NINI UNANG'ANG'ANIA SEHEMU UNAYOFUKUZWA

 HIZI NDIO SABABU ZA KWA NINI UNANG'ANG'ANIA SEHEMU UNAYOFUKUZWA. 

Yawezekana ukawa muhanga kwa sasa au ukawa tayari umepitia hali hiyo na ukikumbuka unajishangaa ni vipi uliweza kuvumilia ilihali ulikuwa unafukuzwa? Au ulipewa dawa? Muda mwingine sio dawa bali kuna sababu ambazo ndio kiini cha somo hili .

Kuendelea kubakia unapofukuzwa kuna hasara nyingi sana japo hasara kubwa sana ni kujipotezea muda wako maana unakuja tena  kuanza moja muda ambao ungekuwa kwenye kumi  na hasara nyingine ya pili kubwa ni gharama ulizotumia kugharamia sehemu isiyo yako .

Inawezekana ikawa ni kazini kwako, sehemu uliyopanga au kwenye mahusiano kote huko huwa tunafukuzwa lakini tunaendelea kupakumbatia na mwishowe tunakuja kukubali ukweli tayari tulishapoteza muda na gharama. 

Kufukuzwa mara nyingi hakuji kama dharura bali huja kwa maandalizi na lazima kuwepo na viashiria viwili vitatu vinavyokuonyesha kuwa upo unafukuzwa . Swali ni je watu huwa tuna upofu kiasi cha kutoona hivyo viashiria vya Kufukuzwa?  Sababu zipo za majibu hayo zipo kwenye somo letu hili la leo .

SABABU ZINAZOFANYA  UENDELEE  KUNG'ANG'ANIA SEHEMU UNAYOFUKUZWA ;

1. KUTOKUBALI MATOKEO; Hapa mtu anakuwa haamini kama kweli fulani anaweza mfukuza au kumkataa hivyo kila siku unakuwa unajipa sababu za kukutia moyo kuwa hilo haiwezekani labda tu ni mabadiliko ya muda mfupi na kesho mambo yatakuwa sawa lakini siku zinazidi kwenda na mambo hayawi sawa hatimaye unakuja kufukuzwa kwa lazima hapo ndipo unagundua kumbe ilikuwa inamaanisha.

2. KUHISI WEWE NDIO UNAMAKOSA MUDA WOTE;Mara nyingi hii hutokea kwenye mahusiano unakuwa unajiona wewe ndio mkosaji hata kwenye makosa yake kwa mfano anaweza kupunguza mawasiliano lakini ukajiona wewe ndio unakosa la kumtafuta na ukimtafuta sana hapokei simu zako wala hajibu jumbe zako unajiona tena wewe ndio mkosaji kwa sababu unamsumbua sana kumbe ndio kiashiria cha kukufukuza hicho ni wewe tu hutaki kuelewa. 

3. KUJIHISI UTAKOSA PAKWENDA: Hii inatokea kote kwenye mahusiano hata kazini unakuwa unahisi ulipata kazi hiyo kwa bahati tu au ulimpata mtu huyo kwa bahati tu ikitokea unatoka hapo huamini tena kama utapata kazi nyingine au utapata tena mtu wa kukupenda. Unakosea sana ndugu yangu usikubali kuvumilia sehemu unayofkuzwa hapo sio kwako tayari ulishafukuzwa sasa kuendelea kuvumilia ni kujiweka kwenye mateso ambayo yange epukika tu kama ungefanya maamuzi magumu na mapema, usikubali kuwa mtumwa ilihali kuna sehemu unaweza kuwa huru kwa maana utakonda bure na hatimaye kupata magonjwa ya kisaikolojia. 

5. Ujinga; Hii ni kama ukosefu wa ufahamu wa kutosha ambapo mtu yoyote anaweza kuwa mjinga kwa kipindi fulani na akajikuta yupo sehemu analazimisha  kujenga nyumba na mtu ambaye usiku anarudi kuibomoa. Jinsi ya kutoka kwenye ujinga ni kutafuta maarifa ya kutosha kuhusu aina ya safari uliyonayo maana ukiijua vizuri aina ya safari yako hutakubali upotezewe muda na msafiri ambaye hamchangii njia moja. 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha.

Pia unaweza pata nakala za vitabu vikakusaidia kukuza ufahamu wako kwa mawasiliano  +255652 134707

Tuesday, 11 April 2023

SABABU ZITAKAZOFANYA UKOSEE KUCHAGUA MWENZI WA MAISHA.

SABABU ZITAKAZOFANYA UKOSEE KUCHAGUA MWENZI WA MAISHA.

Ni jambo la kawaida kuishi wawili( mke na mume) ambapo nyuma ya kuishi pamoja kuna maandalizi ya kumtafuta huyo mwenza hivyo kuna wakati ukifika karibu kila mtu anakuwa na picha ya yupi anamtafuta ndio maana kuna ambao utawakataa na kuna wengine utawakubali , hali ya kumkataa mmoja na kumkubali mwingine ni dalili kuwa kichwani mwako kuna picha ya umtakaye na huyo uliyemkubali ndio picha halisi ya umtakaye, lakini kwa hali isiyoyakawaida kuna kipindi unamchukia uliyemchagua au unaona makwazo kwa aliyekuchagua ilihali yeye ndiye aliyefanya maamuzi ya kukuchagua, hii chanzo chake ni kipi?.

Katika harakati za kumtafuta mwenzi huwa kuna mengi sana nyuma ya zoezi hilo na hapo ndipo huwa kuna kupatia au kukosea zoezi hilo na moja ya sababu hizo ni kama zilivyojadiliwa hapa chini :

Kumtafuta mwenzi kwa ulimbukeni, Limbukeni kwa tafasiri ya haraka ila makinifu ni mtu mshamba au mtu ambaye anakurupukia vitu bila kuwa na ufahamu navyo . Kuna mtu anakuchagua kama mwenzi wake kwa ulimbukeni tu ila kikawaida ingefaa ajitulize sana kabla ya maamuzi yake hayo sasa baadaye mkiwa tayari mpo naye anakuja kugundua kuwa kumbe sio wewe anayekutafuta hapo sasa anaanza kukuchonga ili uwe yule anayemtafuta na hapo ndipo ataanza kukukosoa kila siku .

Kumchagua mwenzi bila utulivu, hii inatokea hasa kwa mtu ambaye anajiona kachelewa hivyo anakuwa haangalii tena vigezo bali anaangalia tu mtu yupi yupo tayari ( kama ni mvulana anaangalia msichana yupi yupo tayari na kama ni mvulana basi anaangalia msichana yupi yupo tayari ) Hapa kukosea ni rahisi sana japo inawezekana ukabahatisha lakini hiyo ni kwa wachache sana wengi hukosea.

Kupitia kipindi cha kukataliwa sana! Mtu aliyepitia kipindi cha kukataliwa sana asipojithibiti kuna uwezekano mkubwa akaja kukosea kuchagua mwenzi kwa sababu atajiona mwenye mkosi sana sasa siku akikubaliwa na yoyote ataona kama bahati hata kama huyo aliyemkubali si sahihi. 

Kufanya maamuzi haraka baada ya kuachwa! mtu anapoachwa huwa hana utulivu na ile hali inamfanya akose utulivu kwa sababu ile hali ya kurudi tena single ( pekee) inampa msongo na anakuwa anataka asionekane hana soko hivyo anaweza kuamua kumkubali yoyote bila kujali ni sahihi au la.

Shinikizo la wengine! Hii ni pale ambapo unataka kuendana na wengine bila kujali kuwa ni wakati sahihi au la bali anataka tu afanye kama wengine kwa mfano marafiki zake wote wameoa bado yeye tu hali hiyo inamfanya na yeye aamue kuoa .

Kukimbia umri! Hii ni sababu nyingine kubwa ya kukosea kwa sababu Kukimbia umri kuna fanya uchague bila kuzingatia ubora wa unachokitaka , na hatimaye kujikuta umekosea. 


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

Kitabu cha siri za urafiki kinapatikana soft copy ( nakala tete) kwa Tsh4000. 

0652 134707/0756388688

Wednesday, 8 March 2023

MWANANGU ! UKIFIKA UGENINI ZINGATIA MAMBO HAYA ILI UFANIKIWE 

 MWANANGU ! UKIFIKA UGENINI ZINGATIA MAMBO HAYA ILI UFANIKIWE 

Kila mtu kwa sehemu ni lazima kawahi kuwa mgeni au atakuwa mgeni tu siku moja,kuwa mgeni haiepukiki kila mtu ni lazima atapitia, yawezekana ni ajira mpya au kutoka nyumbani kwenda mkoani kutafuta maisha. Wengi tukifika ugenini huwa tunajikuta kwenye migogoro mingi na wenyeji kiasi cha kuchukia kabisa eneo hilo na hatimaye kushindwa kufanikisha lengo kuu lililotupeleka ugenini, Uhaba wa ufahamu wa mbinu za kuishi ugenini ni sababu kubwa za yote hayo ndio maana nikaona nikuandalie machache yatakayokusaidia kuishi ugenini kwa mafanikio makubwa.Ukifika ugenini zingatia haya :

1.Usifike ukawa mjuaji kuliko wenyeji uliowakuta kwani watashindwa kukuonyesha hata kisima cha maji kilipo.

2.Usifike na kuanza kukosoa wenyeji kwani wataona unawadharau.

3.Usifike ukaanza kudharau kabila la wenyeji tena hili ni kosa kubwa ukifika epuka maongezi yanayotaja makabila ya watu au kutolea mifano makabila ya watu.

4.Ukifika tafuta nyumba ya ibada na jumuiya jiunge huko kwa sababu watakaokusaidia kwa huduma ya kwanza ni hao wenyeji na sio kwenu ulipotoka , hata kama kwenu wana uwezo vipi wa kifedha lakini kuna shida zako nyingine wao watakwama lakini wenyeji wako watazimudu. 

5.Usianzishe mahusiano ya kimapenzi haraka haraka, kuwa mtulivu.Hata kama umefika na ukamuona mtoto wa mtu ukampenda sana jitahidi ujizuie tena hapo jizuie haswa kwa sababu hujui mengi kumuhusu huyo binti yawezekana asiwe na shari yoyote lakini kumbe tayari ni mchumba wa mtu hapo ugenini hivyo ukajikuta kwenye vita na wenyeji na huwezi kuishinda hiyo vita kwa sababu utapigana na wanaojua ghara za silaha zilipo. 

7.Usionyeshe ukubwa wako acha waone kwa vitendo.Usifike ugenini ukaanza kuonyesha ukubwa wako au ukaanza majisifu wewe fanya kilichokupeleka kwa weredi na bidii zote na kama una huo ukubwa basi utaonyeshwa na juhudi zako.

8.Acha wenyeji watawale mazungumzo hata kama unaongea kama chiriku jizuie 

9.Usiwaonyeshe kuwa wewe ni bora zaidi yao hata kama ni kweli jifanye tu mwanafunzi hata kama wewe ni mwalimu.

10.Usinunue ugomvi acha wachukiane wao wewe kaa pembeni Ukifika utaanza kuonyeshwa nani mbaya na nani mzuri tafadhali usikurupuke kuunga mkono upande mmoja wapo bali tulia tu na baadaye utajionea mwenyewe nani anafaa na nani hafai. 

11.Hata kama una pesa anza kwa kula vyakula vyao 😄 Namaanisha ndio usifike ukaanza kuona kama vile vyakula vyao havifai na hata kama wanatumia usichoweza kula basi usikatae kwa dharau bali tumia hekima kubwa kufikisha ujumbe kuwa chakula chao ni kizuri sana na tena unasikitika kukikosa lakini huna namna inabidi tu ukikose.

12.Una elimu kubwa ndio lakini ukifika ugenini usigombanie uongozi ,wenyeji watakuchukia haraka watajua umeenda kuharibu maslahi yao .Ukifika kubali kuongozwa na tii kila kiongozi wako bila kujali unamshinda nini, baadaye wakiona unafaa wao wenyewe watakupa uongozi.

13.Sio lazima uwe kiongozi eneo hilo yawezekana nafasi yako nzuri ni kuwa mshauri wa viongozi wa eneo hilo.


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha. 


#kitabu cha thamani ya changamoto kinapatikana nakala tete ( soft copy)

+255652 134707




#kitabu cha thamani ya changamoto kinapatikana 

+255652 134707

Sunday, 26 February 2023

HIVI NAWE UNAFANYA MAMBO KWA HASARA? 😔 KAMA JIBU NI NDIO, MAKALA HII  INAKUHUSU 

 HIVI NAWE UNAFANYA MAMBO KWA HASARA? 😔 KAMA JIBU NI NDIO, MAKALA HII  INAKUHUSU .

Japo wataalamu wanasema hakuna kipimo cha muda sahihi wa mafanikio lakini vipo vipimo vya kujipima kuwa unafanya mambo kwa hasara na ukijua hilo itakuwa rahisi kufanya maamuzi magumu ya kutoendelea na shughuli hiyo inayokupa hasara au kujiboresha ili upate uanze kupata faida.  Inaumiza sana kutumia nguvu kubwa halafu matokeo yaje kidogo au yasije kabisa 😔  Bahati mbaya ni kuwa wengi huwa hatujitambui kuwa tupo tunapoteza muda bure bali tunakuwa tunajifariji kuwa tupo tunavumilia na ipo siku tutafanikiwa, sio vibaya kujipa faraja lakini ni vibaya pia kujipa faraja kwenye sehemu isyo yako au kujipa faraja kwa kitu ambacho haiwezekani.Somo hili lipo mahususi kwa watu ambao wanasumbuka na changamoto ya kufanya mambo kwa hasara.

Zipo dalili nyingi za kujipima ili kujifahamu kuwa upo kwenye kundi la watu ambao hufabya mambo yao kwa hasara, dalili hizo ni kama zifuatazo;

1. Unafanya mambo bila kuyamaliza , kwa mfano leo unaanza safari ya kusoma kabla ya hujamaliza miaka yako ya ki elimu unaona kuwa umekosea unaachana na kozi hiyo na kutafuta kozi nyingine 😔 Unafungua biashara fulani na kabla hujaimudu vyema unajiona kuwa umekosea unaifunga na kuanzisha nyingine 😔 Unaanzisha mahusiano ya kimapenzi kwa furaha zote lakini ndani ya muda mfupi unaona umekosea unamuacha na kutafuta mwingine 😔 

2. Unakaa hatua moja kimafanikio kwa muda mrefu bila kuhama,hii hutokea pale ambapo mbele husogei kwa mfano unauza biashara ya nyanya miaka na miaka na kwa mtaji ule ule  .

3.Unafanya jambo bila kuwa na muda wa ukomo kwa mfano  unaamua kufanya biashara ya kutembeza mitumba ya n  lako la nguo na uachane na kutembeza mtaani. 

4. Upo kwenye mahusiano  na unaona kabisa ishara zote kuwa hutakiwi hapo lakini unaendelea kuvumilia kwa sababu unaona utakosa pakwenda  , hii ni dalili ya kuwa unafanya kihasara. 

Je kuna dalili moja wapo unayo hapo juu? Au zifananazo na hapo? Kama jibu ni ndio basi upo unafanya vitu bila mafanikio , je utatokaje? 

Njia rahisi ya kutoka kwenye kufanya mambo yasiyo na mafanikio ni kuwa na muda wa kutosha wa kujitathmini kwenye chochote ufanyacho na kujitengea ukomo wa muda usikubali ukae eneo moja muda wote la sivyo iwe ndio mwisho wa malengo yako  kama sivyo jiwekee muda wa kutoka hapo kama unauza maji ya basi moja uwe na kiwanda cha kutengeneza maji . Jiwekee mbinu za kujifanyia uchunguzi kila muda fulani.


Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

+255652134707

Saturday, 14 January 2023

 HIZI NDIO SABABU ZINAZOFANYA UWE MTU WA KUJUTIA MAAMUZI YAKO

 HIZI NDIO SABABU ZINAZOFANYA UWE MTU WA KUJUTIA MAAMUZI YAKO 


Na Mwanasayansi Saul Kalivubha ✍ 


Ulijawa na furaha siku hiyo na hata kama angetokea mtu wa kukwambia kuwa unachotaka kufanya ni hatari pengine ungemuona ni adui asiyependa mafanikio yako lakini furaha yako leo haipo tena 😞 Unajutia  maamuzi yale .Kwa nini umekuwa mtu wa kujutia maamuzi yako ? Na ilihali jana ulijiona upo sahihi kwa maamuzi hayo? Twende darasani. 

Maamuzi ni eneo muhimu sana kwenye maisha yetu kwa sababu maamuzi ndio miguu yetu ya kutembelea , upo hapo ulipo leo  kwa sababu kuna maamuzi uliyafanya jana na hata hao unaowashangaa leo wapo hivyo kwa sababu kuna maamuzi waliyafanya jana .

Kujutia sio kitu kigeni kwa sababu karibu kila mtu ana siku moja au zaidi za kujutia maamuzi yake, hakuna ambaye hajawahi kujutia katika maisha yake lakini wapo watu ambao kwao ni zaidi yaani kwenye maamuzi kumi waliyofanya basi   zaidi ya maamuzi matano kwao sio sahihi ni lazima wayajutie.

Kwa nini leo ujione umekosea na wakati jana ulijiona sahihi kwa maamuzi yale yale?  Yapo mambo mengi ambayo yanachangia hali hiyo kutokea  na vizuri uyafahamu mambo hayo ili ujue namna ya kupunguza majuto , na kama unakuwa mwingi wa majuto kuna uwezekano mkubwa ukawa ni mtu ambaye huna furaha kwenye maisha yako kwa sababu unakuwa unafikiria  yaliyopita tu .

Ufahamu wako wakati wa maamuzi ni sababu kubwa sana ya majuto kwa wengi, wajua ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu kinachofanya uamue ni Ufahamu wako wa muda huo hivyo kama ufahahamu wako ni mdogo sana basi hata maamuzi yako kwa asilimia kubwa  yatakuwa sio bora pia na siku ufahahamu wako ukikua ni lazima utaona kuwa ulikosea maamuzi . Tunajutia maamuzi yetu ya jana kwa sababu tuliyafanya tukiwa na ufahahamu mdogo tofauti na leo tulivyo kwa mfano  kama jana ulifanya maamuzi ya kuacha shule kwa ufahahamu kuwa shule inakupotezea muda  ni bora ufanye biashara lakini ulipoanza biashara ukakutana na changamoto zikakumbusha kuwa kuna kiwango cha elimu kinatakiwa ili uweze kuimudu hiyo biashara na hapo ndipo utaaanza kujiona ulikurupuka kwenye maamuzi. 

Matokeo ya maamuzi yetu tuliyoyafanya jana ndio yanasema na sisi leo kutu onyesha ni jinsi gani tulikosea/kupatia  kwenye maamuzi yetu hayo , kuna kanuni moja ya kimaamuzi inasema kuwa kila maamuzi uliofanya ni lazima matokeo yake yaje kusema na wewe siku moja na hapo ndipo utagundua ni jinsi gani ulikuwa sahihi. Matokeo hufanya watu tujifahamu vizuri tukoje na kama utakuwa mtu chanya basi utatumia matokeo hayo kujifunza. 

Mihemko pia ni sababu nyingine inayofanya tukosee maamuzi kwa sababu maamuzi yako yatakuwa ni matokeo ya hisia za muda mfupi tu zisizo na fikra ndani yake ndio maana unashauriwa kuwa na utulivu kabla ya maamuzi japo kuna maamuzi mengine ni lazima tuyafanye kwa haraka kulingana na uhitaji wake lakini hayo ni kama dharura  tu ila maamuzi mengi lazima kuna muda utapata wa kufikiria hivyo kabla hujaamua jitahidi huna mihemko . Mihemko mara nyingi chanzo chake ni kukosa utulivu na muda mwingine kuchochewa na mazingira ya nje ikiwemo kuishi kwa kujilinganisha sana. Ukiishi kwa kujilinganisha utakuwa mtu wa kujiona umechelewa kwenye maisha na mwishowe utaanza kufanya vitu bila utulivu .

Kushindwa kuitawala shauku yako pia ni sababu inayoweza kukufanya ukosee maamuzi kwa sababu utakuwa mtu wa kukurupukia mambo kabla ya wakati wake ili tu ukidhi shauku yako Maamuzi yako Hayawezi kuwa sahihi kama unayafanya kwa shauku ambayo haikudhibitiwa .

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

Mitandaoni tunapatikana kwa jina la fikiandotozako. 

Pia kitabu cha namna ya kudhibiti mwili kinapatikana kwa soft copy Tsh 3000 

+255652134707

Sunday, 8 January 2023

JIFUNZE TOFAUTI KATI YA WIVU NA KUTOJIAMINI

 JIFUNZE TOFAUTI KATI YA WIVU NA KUTOJIAMINI KWENYE MAHUSIANO 

Na Mwanasayansi Saul Kalivubha ✍ 

Wivu kwa maana rahisi ni kutojiamini , unahisi kuna watu wenye sifa zaidi yako watakuibia mpenzi wako 😔 Wivu hukoleza mapenzi 😊 

Kutojiamini ni wivu uliopitiliza kiasi , muda wote unahisi umpendaye ana njama mbaya dhidi yako kiasi cha kila siku kuwa na migogoro isiyoisha 

Kutojiamini ni sumu ya mahusiano.Wafikiri sababu zake ni nini? Na utajijuaje ikiwa una tatizo hili ?  Karibu darasani 

DALLI ZA KUTOJIAMINI 

Asipojibu meseji kwa wakati tayari unahisi kafanya makusudi 😔 

Asipoitikia simu yako wewe unajua yupo anafanya kitu kibaya 😔 

Ukimpigia simu akiwa anaongea na mtu mwingine tayari unahisi yupo anakusaliti 😢

Siku haiishi bila kumuwazia mabaya yaani unahisi kama vile hakupendi au anakudharau 😔 

Muda wote unahisi kama anakudanganya tu hakuna siku unamuamini 😔 

Unakuwa mwepesi kukasirika kwa vitu vidogo vidogo tu

Hujui bahati mbaya kila kitu kwako unaona ni njama mbaya aliyoipanga kukufanyia 😔 

Akiwa na marafiki zake tayari unahisi anakusaliti au wanamshaurii mabaya kukuhusu wewe 😔


Weka alama ya tick kwenye dalili inayokusumbua ikiwa kila migogoro ya mahusiano yako chanzo ni dalili zaidi ya nusu kati ya hizo kuna uwezekano mkubwa kati yenu kuna tatizo la Kutojiamini .Kutojiamini kuna leta migogoro na ni ngumu kuwa na mahusiano yenye afya nzuri ikiwa kati yenu kuna migogoro ambayo chanzo chake  kikubwa ni Kutojiamini .

Mbona hata dalili za wivu ni kama zinafanana na za Kutojiamini?  Swali zuri sana hilo ni kweli kabisa dalili pia za wivu ni kama hizo hizo sema kama nilivyokwiaha kusema juu kwenye utangulizi kuwa wivu ni Kutojiamini kuliko na kiasi na huwa hakuna migogoro kwenye wivu wa mapenzi bali hukuza mahusiano yenu ya mapenzi , bila wivu wa kiasi mahusiano huwa hayana raha. 


Kwenye wivu kuna upendo lakini kwenye kutojiamini  kuna upendo wa mashaka ndio maana kutojiamini ni chanzo kingine cha kuvunja mahusiano au kufanya watu wakuogope kwa sababu tu ya migogoro kila siku, hakuna anayependa migogoro ya kila siku .

Kutojiamini chanzo chake ni nini?  Kuna vyanzo vingi vya tatizo hilo yawezekana ikawa ni sababu za kimazingira au za kuzaliwa nazo( kurithi). Tuone sababu chache zifuatazo:

Kuwa na historia ya kusalitiwa : Mara nyingi tatizo la Kutojiamini linaonekana kwa watu ambao wana historia ya kusalitiwa na wenzi waliowapenda sana hivyo wanakuwa hawana imani tena watu , na mara nyingi tatizo linakuwa kubwa kama muhusika ataamua kuingia kwenye mahusiano mapya bila kupona kwa jeraha lake la kwanza hivyo matokeo yake anakuwa anaishi na mtu wa pili kama vile ni mtu yule wa kwanza.Tiba ya  tatizo hilo ikiwa chanzo ni hiki basi tiba yake ni kujiponya majeraha kabla ya kuingia kwenye mahusiano mapya. 

Chanzo kingine ni tabia yako ya kutafuta ukamilifu wa 100%; Tatizo hili ndio chanzo cha kutoamini kuwa kuna bahati mbaya ndio maana mwenzio akifanya vitu bahati mbaya tayari unajua ni makusudi kakufanyia na tayari ni mgogoro huo , hutaki kumuona kama na yeye ni binadamu bali unamuona kama ni malaika ambaye hakosei hata kidogo.  Tiba yake hapa  ni kujifunza kupuuzia baadhi ya vitu vinavyotokea kwenye mahusiano yako muhimu tu visiwe vina madhara makubwa kwenye safari yenu , kuna mambo unaweza kuyapuuzia na yasilete madhara kwenye mahusiano yenu lakini ukikata kufuatilia kila kitu lazima mtakuwa na migogoro mingi sana kwenye mahusiano yenu .

Chanzo kingine ni kuathiriwa na huyo umpendaye yaani unayempenda anakuwa na historia ya kukusaliti hivyo tayari kumuamini tena inakuwa ngumu hivyo anakujengea tabia ya Kutojiamini tena na matokeo yake ni kuwa na mashaka dhidi ya matendo yake. Tiba ya hapa inachukua muda wa kutosha na lazima yeye ndiye akutibu kwa kukuaminisha kuwa kaacha tabia zake za awali .

Chanzo kingine ni urithi; Tayari umezaliwa upo hivyo tu yaani una tatizo la Kutojiamini la kuzaliwa nalo , hapa kuna tiba kutoka pande mbili ambazo ni kutoka kwako na anayekupenda. Lazima ujikubali kuwa una tatizo na kujidhibiti pale uwezapo  na huyo akupendaye inabidi ajue kuwa una kasoro hiyo Hivyo lazima ajifunze kuishi na wewe. 

Makala hii imeandikwa na Mwanasayansi Saul Kalivubha 

Mafunzo yetu yapo mitandaoni kote kwa jina la fikiandotozako 

Pia kitabu cha siri za urafiki kinapatikana soft copy ( nakala tete) kwa Tsh4000 tu , ukilipa utatumiwa muda huo huo 


+255652 134707